Thursday, June 28, 2012

Kupotoshwa Idadi ya Waislamu ni Changamoto kwa Waislamu!



  • Ni ipi ajenda ya walioficha na kupotosha  idadi yaWaislamu?
  • Waislamu himizaneni kushiriki kwa wingi katika sensa ijayo 
  Na Ahmed Hussein
Hila dhidi ya idadi ya Waislamu katika koloni la Tanganyika zilianza siku nyingi. Hili ndilo koloni lililobeba idadi kubwa ya Waislamu katika Ukanda wa Afrika Mashariki. Idadi hii ilionekana kuwakera wakoloni na washirika wao wa kimeshari. Itakumbukwa kuwa Wakoloni walibuni mkakati wa kushamirisha miradi ya ufugaji wa nguruwe ili kuwafukuza Waislamu katika maeneo yao.
Hujuma za kitakwimu dhidi ya idadi ya Waislamu Tanzania ni za miaka kama si miongo mingi. Idadi ya Waislamu nchini ilianza kugubikwa na wingu jeusi hata kabla ya uhuru. Kwa makusudi, mamlaka za hesabu za watu ziliondosha utambulisho wa kidini katika sensa bila sababu za wazi.

Kumbe ukweli uliokuwa umefichwa ni kwamba idadi ya Waislamu ilikuwa kubwa kuliko ya makundi mengine. Ukubwa wa idadi ya Waislamu ulitofautiana mno na uwakilishi wao katika maeneo ya elimu hasa kuanzia ngazi ya sekondari, na katika nyadhifa za utumishi wa umma na madaraka serikalini.
Swali ambalo lilikuwa likiogopwa kitakwimu ni kwamba laiti sensa ingefichua idadi kubwa ya Waislamu nchini, hoja ya msingi ingekuwa hii; kwa nini kielimu na kimadaraka Waislamu walikuwa wachache?
Wabunifu wa Mfumo uliojengwa kwa misingi ya dhuluma dhidi ya kundi la Waislamu katika jamii ya Watanzania waling’amua kuwa mikakati yao ya kuwapunja Waislamu taaluma na madaraka ingefichuka kirahisi kama sensa ingeonesha idadi kubwa ya Waislamu nchini.

Hivyo, kwa maslahi ya mkakati huo wa dhuluma, ilibidi wafiche Idadi ya makundi ya dini ili umma usije kuhoji mbona katika daftari la sensa Waislamu ndio wengi lakini katika nafasi za elimu, utumishi na madaraka ni wachache?
Wakati vigezo vya sensa vya Umoja wa Mataifa vinajumuisha utambulisho wa dini, Tanzania licha ya kuwa mwanachama wa Umoja huo, ikakiuka utaratibu huo wa kuweka wazi hesabu za watu wa makundi ya dini. Kwa bahati mbaya, mwamko kwa Waislamu ulikuwa bado mdogo au hafifu juu ya ajenda ya kuondosha utambulisho wa dini katika sensa za Kitaifa, hivyo, jambo hilo halikupigiwa sana kelele.

Laiti ingetosha kuwa, Idadi za Watu wa makundi ya dini hazifahamiki kwa sababu hazijumlishwi kupata wastani katika daftari la sensa, huenda kila mmoja angeamini kuwa uamuzi huo ulikuwa wa kizalendo.
Lakini ajabu ambayo imeonekana Kitaifa na Kimataifa ni kwamba, taasisi kadha wa kadha zimekuwa zikitoa au kutumia takwimu zinazoonesha kuwa kundi la Wakristo ndilo linalounda jamii kubwa ya Watanzania likifuatiwa na lile la Waislamu!
Hiyo ni kusudi ya wabunifu au tuseme waasisi wa mfumo kandamizi uliohujumu nafasi ya Waislamu kielimu na kiutumishi katika nyadhifa za juu na madaraka. Kwa nini walifanya kusudi hiyo? Kwa sababu walitaka jamii na dunia iamini kuwa uchache wa Waislamu katika maeneo hayo ni matokeo ya uchache wa idadi ya jumla!

Hiyo pia ingetoa picha ya jumla kuwa uchache wa Waislamu unaooneshwa na takwimu bandia ndio sababu ya uchache wao kielimu na kimadaraka. Au pia uchache wao kielimu na kimadaraka ni ushahidi wa idadi yao ndogo katika jamii ya Watanzania.
Hivyo, kama yalivyo makundi mengine madogo ya jamii, uwakilishi mdogo wa Waislamu katika maeneo muhimu ya nchi unaakisi “udogo” wa jamii yao

Waliofanya kusudi hiyo ya kupotosha takwimu walikuwa na uhakika wa kuteka asilimia 100 ya saikolojia ya walimwengu juu ya uwiano pogo wa kielimu na kimadaraka baina ya watu wa makundi ya dini iwapo sensa ingeficha utambulisho wa dini ili isijulikane Waislamu wako wangapi Tanzania.
Kwa upande mwingine, upotoshaji wa takwimu kuwa Wakristo ndio wengi nchini ulilenga, pamoja na mambo mengine, kuhalalisha dhulumu ya kimfumo dhidi ya Waislamu katika maeneo ya elimu na ajira za utumishi wa umma hasahasa katika ngazi za juu. Kwamba, wingi wa Wakristo katika maeneo hayo ni matokeo ya ukubwa wa idadi yao kulinganisha na makundi mengine ya jamii.

Ni hoja nyepesi kung’amulika kwamba kama wasingetoa takwimu za kuonesha kuwa Wakristo ndio wengi nchini, wabunifu na waasisi wa mfumo kandamizi wa kidini kwa misingi ya kisiasa wangeyajibu vipi maswali haya; ‘mbona Waislamu ni wachache katika maeneo hayo? Je wingi wa Wakristo mashuleni, vyuoni na madarakani umetokana na nini?
Mwanzo, ilidaiwa kuwa mfumo wa Kikoloni uliwabana Waislamu kielimu kwa sharti la kuritadi ili wapewe elimu, sawa kabisa, mtu angekubali kuwa katika miaka ya awali ya uhuru nafasi za madaraka zingejazwa na Wakristo waliopendelewa kielimu na mkoloni.
Lakini hoja ambayo ingewashinda Wabunifu wa mfumo wa dhuluma ni kwamba mbona hata baada ya uhuru Waislamu wameendelea kuwa wachache katika nyanja za elimu? Kama nyuma kulikuwa na sharti la kubatizwa, je baada ya uhuru sharti hilo lilikuwepo? Lakini bado hilo nalo lingesutwa na idadi ya watoto wa Kiislamu katika shule za msingi.
Waislamu waliandikisha watoto wao kwa wingi katika ngazi ya msingi nchini kote. Sasa, swali lingekomaa zaidi, kwa nini Waislamu waendelee kuwa wachache hata baada ya miaka mingi ya uhuru? Ni wazi mfumo wa dhuluma ungebainika kirahisi.

Ndio maana waasisi wake wakawa makini na sensa ya Taifa ili wajenge hoja ya jumla kuwa Waislamu ni wachache katika nyanja za elimu na madaraka kwa sababu jamii yao ni ndogo kama zilivyo jamii za watu wa makundi mengine madogo.
Na Wakristo ni wengi kwa sababu wao ndio wanaounda asilimia kubwa ya Watanzania. Angalau kwa kuficha takwimu za Waislamu walijiridhisha kuwa dhuluma waliyowafanyia Waislamu ingehalalika kwa mdadisi au mtafiti yeyote yule ambaye angetaka kuhoji kwa nini Waislamu ni wachache madarakani?

Mfano ambao ungetia nguvu dai hilo ni ule wa nchi nyingine jirani kwamba huko Wakristo ndio wengi madarakani kwa sababu jamii ya Waislamu ni ndogo kwa idadi. Jitihada za kuficha takwimu za Waislamu katika sensa ya Taifa, zilikuwa na ajenda ya kutoa picha ya Kimataifa kuwa katika ukanda wa Afrika Mashariki Kanisa ndilo lenye wafuasi wengi katika nchi zote.
Hivyo, isishangaze kuona Waislamu wachache wakiwa madarakani Tanzania kwani hali ndiyo hiyo hiyo katika nchi jirani za eneo hilo. Kwa kweli, dunia imehadaika sana kwa hila hii. Sehemu kubwa ya watu duniani wakiwemo baadhi ya Watanzania wanaamini kuwa ukiondoa Zanzibar, Waislamu, Tanzania bara, ni wachache kulinganisha na Wakristo.

Tangu hapo, Tanzania ni Taifa la Kikatoliki kwa kauli ya Mwalimu Nyerere. Ili kujenga picha ya kuhalalisha Ukatoliki lazima, kimsingi, upotoshe takwimu za Waislamu ili idadi ya Wakristo ionekane kubwa na hivyo inafaa kuwa Jimbo la Vatikani.
Ingekuwa rahisi kutumia takwimu sahihi za Wakristo na Waislamu wa Kenya kuhalalisha himaya ya Kanisa kwa sababu ni kweli idadi ya Wakristo kule ni kubwa. Lakini isingeliwezekana kujenga himaya ya Ukatoliki kwa kutumia takwimu sahihi za sensa ya Taifa ya Tanzania kwani ingeonesha idadi kubwa ya Waislamu.

Kwa sababu hiyo, mkakati ukawa ni kuficha na kupotosha takwimu. Kuficha kuna maana ya kuondosha utambulisho wa dini katika sensa, na kupotosha kuna maana ya kusambaza takwimu bandia za idadi ya watu wa makundi ya dini. Hebu tazama jedwali hili
                    
s/no

Nchi

Idadi ya Waislamu


Idadi kwa asilimia

Makadirio hadi 2030

Makadirio kwa asilimia

43
*TANZANIA*
“13, 450, 000”?
 ‘29.9’
“19, 463, 000”?
 25.8













Katika jedwali ambalo niliwahi kuchapisha katika makala iliyohusu upotosha wa takwimu za idadi ya Waislamu Tanzania, Tanzania iliorodheshwa katika nafasi ya 43 kama kinavyoonesha kipande cha jedwali hilo hapo juu. Jedwali hilo linaonesha kuwa eti idadi ya sasa ya Waislamu ni milioni 13, 450, 000 sawa na asilimia 29.9 ya Watu wote Tanzania!

Kana kwamba upotoshaji huo haukutosha, jedwali hilo likaonesha makadirio yaliyofanywa na taasisi za Kimataifa kwa kushirikiana na mtandao usiofahamika kuwa eti hadi utakapofika mwaka 2030 yaani miaka 28 ijayo kuanzia sasa, idadi ya Waislamu Tanzania itakuwa ni milioni 19, 463,000 sawa na asilimia 25.8 ya idadi ya watu wote Tanzania.
Niliandika na kuchapisha jedwali hilo kwa minajili ya kuwaandaa Waislamu kisaikolojia na kimkakati kwamba waitumie sensa ijayo
kusahihisha upotoshaji huo. 

Na jambo la kung’ang’ania ni kwamba sensa hiyo ya Mwezi Agosti mwaka huu lazima ijumuishe utambulisho wa kidini.
Hiyo ikiwa na maana kuwa lazima daftari liwe na kipengele cha dini ya mtu anayehesabiwa. Kwa bahati nzuri, Umoja wa Mataifa ndio umeweka kigezo hicho, na Tanzania ni mwanachama wake, hivyo isidhaniwe kuwa kudai kigezo hicho ni ‘udini’.
Ni jambo la kusikitisha kuwa baadhi ya Waislamu walioitolea maoni makala yangu ile walipuuza umuhimu wa sensa kwa madai kuwa ‘Uislamu haujali idadi ya watu’ bali unajali waumini. Hii si dalili nzuri kwani ‘uumini ni daraja’ na Uislamu ni utambulisho.
Maadam mtu katoa shahada ya kumkubali Mwenyezi Mungu na Mtume, hebu tumuhesabu kuwa ‘amesilimu’ kama inavyosema Qur’an. Tusimpime kwa daraja la uumini ambalo chujio lake kali pengine linaweza kubakisha watu wawili au watatu kwa ile mizani hasa ya uchaMungu.

Huenda mimi na msomaji tusiwemo katika daraja hilo japo tunaswali na kufunga. Naomba tuamini kuwa “sensa ya Waumini” ni tofauti kabisa na “sensa ya Waislamu”. Kwa hiyo, tusisitize sensa ya Waislamu katika daftari la sensa ambayo itawajumuisha Waislamu wote bila kujali daraja zao za imani.

Monday, June 25, 2012

Mchakato wa Katiba Mpya Maelekezo Kwa Waislamu


KITABU:Mchakato wa Katiba Mpya Maelekezo Kwa Waislamu
JUKWAA LA WAISLAMU LA KURATIBU MCHAKATO WA MABADILIKO YA KATIBA TANZANIA  
(JUWAKATA)
 MUHIMU KWA WAISLAMU WOTE

Yaliyomo.
1. Ijue JUWAKATA
2. Maelezo ya awali
3. Katiba ya nchi ni nini?
4. Aina za Katiba duniani
5. Muundo na vipengele vya katiba ya Tanzania
6. Hatua za mchakato wa kupata katiba mpya

  • Tume ya kurekebisha Katiba
  • Bunge la Katiba
  • Kura ya Maoni
7. Kwa nini Waislamu wanashiriki katika mchakato wa katiba?
  • Wajibu      wa kupigania haki
  • Uislamu      na katiba
  • Fiq-hi      na mazingira yaliyopo
  • Wajibu      wa Viongozi Waislamu
  • Wajibu      wa Wanataaluma Waislamu
  • Wajibu      wa Muislamu mmoja mmoja
  • Umakini      wetu
8. Mambo ya kupiganiwa na Waislamu katika katiba mpya.
9. Hitimisho.





1. JUWAKATA

JUWAKATA ni Jukwaa la waislamu la Kuratibu mchakato wa Mabadiliko ya Katiba Tanzania. Chombo hiki kinaundwa na Jumuiya na Taasisi mbali mbali za Kiislamu sizizopungua 40. Chombo hiki kilizinduliwa rasmi katika kongamano kubwa lililohudhuriwa na kada mbalimbali za Masheikh, wanataaluma na viongozi wa Kiislamu lililofanyika Januari 6, 2012 katika ukumbi wa Diamond Jubilee Jijini Dar es Salaam na kuhusisha vyombo mbalimbali vya habari. Makao makuu ya JUWAKATA ni Dar Es Salaam. JUWAKATA lina mawasiliano ya karibu na Waislamu wa Tanzania Visiwani kwa uratibu wa pamoja.
Aidha azimio la mkutano mkuu wa Jumuiya na Taasisi za kiislamu, limeipa JUWAKATA idhini ya kushirikiana na muislamu au mwananchi yeyote mwenye malengo ya kupatikana katiba yenye misingi ya haki na uhuru pasina ubaguzi wa aina yoyote.
  1. MAELEZO YA AWALI
Nchi yetu imo katika mchakato wa mabadiliko ya katiba ya nchi. Wananchi wa Tanzania wanakabiliwa na jukumu moja la kuhakikisha katiba ijayo itakuwa kwa maslahi ya watanzania wote na yenye kuzingatia haki na usawa bila kujali kabila, rangi, dini wala jinsia. Tukio la kuundwa kwa katiba ya nchi ni miongoni mwa matukio makubwa kabisa katika nchi yoyote ile duniani. Ni kwa sababu hii, mivutano, ushindani, kupigana vikumbo, mizengwe na mahala pengine vita vya wenyewe kwa wenyewe hutokea. Ni kwa kutambua ukweli huu, sisi waislamu wa Tanzania, tayari tumekwisha ipatia ushauri serikali ya Jamuhuri ya muungano wa Tanzania na Tume ya kurekebisha katiba tahadhari ya kuzingatiwa haki na uadilifu katika mchakato wote wa mabadiliko ya katiba ili katiba iwe kwa faida  ya wote na iwe msingi wa kudumisha amani iliyopo.
  1. KATIBA YA NCHI NI NINI?
Katiba ya nchi  ni makubaliano ya wananchi kuhusu haki na wajibu mbali mbali kati ya dola na raia na jinsi ya mgawanyo wa madaraka na rasilimali za taifa, mfumo wa utoaji haki na ulinzi na usalama wa nchi.
Kutokana na ainisho hili la ujumla, makubaliano haya ya katiba yanaweza kuwekwa katika maandiko au yasiwekwe. Hata hivyo nchi nyingi duniani zinaongozwa kwa katiba iliyoandikwa. Mara nyingi tumepata kusikia kwamba ‘katiba ndiyo sheria mama ya nchi’. Hii ni kutokana na ukweli kwamba, sheria na kanuni mbali mbali zinazoongoza nchi chimbuko lake ni katiba.
Katiba hujumuisha mambo makubwa ya kisheria ambayo huandikwa kwa mukhtasari. Kwa mfano kipengele kimoja kinacho zuia ubaguzi, kinaweza kukusanya mambo lukuki yanayohusu ubaguzi wa rangi, jinsia, dini, ukabila, umri, hadhi katika jamii nk.  Kwa muktadha huo Bunge la nchi ndicho chombo kinachoundwa na katiba kwa madhumuni ya kutunga sheria, kanuni mbali mbali ili kufafanua jinsi ya kutekeleza vipengele vya katiba husika. Sheria na kanuni ambazo hutungwa na Bunge, ikiwa zitapingana na katiba ya nchi, sheria hizo huhesabika kuwa ni batili (yaani null and void).
  1. AINA ZA KATIBA DUNIANI
Katiba zimegawanyika katika mafungu makubwa mawili.
  • Katiba za kisekula na
  • Katiba ya Kiislamu.
Katiba za kisekula zimebeba taswira kubwa mbili:
(a) Katiba za kidikteta na
(b) Katiba za kidemokrasia.
Katiba za kidikteta ni zile ambazo wananchi hawana kauli juu ya mambo ya uendeshaji wa nchi yao wala hawaruhusiwi kuchagua wawakilishi wao bali mamlaka na madaraka yote ya nchi yako mikononi mwa mtu au tabaka la watu wachache.
Katiba za kidemokrasia ni ile ambayo wananchi wanashirikishwa katika kuamua nchi yao iendeshwe namna gani na wanashiriki katika kuiendesha nchi kwa kuchagua wawakilishi wao.
Katiba ya Kiislamu – Hii hutokana na Qur’an na Sunnah za Mtume (SWALALLAH ALAYHI WASALLAM) na Ijmaa ya wanazuoni. Wananchi hulazimika kutii na kutekeleza mipango na ibada nyingine kwa kadiri ya uwezo walio nao. Watawala wa Kiislamu huongoza na kutoa hukumu kwa kila jambo kwa kuzingatia mwongozo wa Allah (Subhaanahu Wataala) na Sunnah za Mtume (SWALALLAH ALAYHI WASALLAM).
5. MUUNDO NA VIPENGELE VYA KATIBA YA TANZANIA
Muundo wa dola ya Tanzania kwa mujibu wa Katiba ya sasa ni wa ushirikishwaji wa wananchi katika uendeshaji wa nchi kupitia wawakilishi (wabunge, wajumbe wa baraza la wawakilishi na madiwani). Katiba ya Tanzania ina sehemu kuu kumi (10) na ibara (152) kuhusu mambo mbali mbali.
Katika sehemu zake kumi (10) na ibara (vifungu) 152 katiba ina sehemu zinazoeleza misingi ya katiba, muundo wa dola, mipaka ya nchi, vyama vya siasa, sera ya nchi, haki za raia na wajibu wao, majukumu ya Serikali, Bunge, Mahakama nk.  Kwa ujumla kutokana na muundo huu wa katiba ya Tanzania, katiba iliyopo sasa inahesabika kuwa ni miongoni mwa ‘katiba za kidemokrasia’.
6. HATUA ZA MCHAKATO WA KUPATA KATIBA MPYA
  • Kupitishwa kwa Sheria ya mabadiliko ya Katiba
Hatua hii ilifikiwa mnamo mwezi wa Novemba, 2011 pale muswada wa Sheria Na. 8 ya mabadiliko ya katiba, 2011 ulipopitishwa na Bunge. Kisha yalifuata marekebisho ambayo yalifanyika Januari, 2012. Sheria hii ya mabadiliko ya katiba, ndiyo inayotumika kuongoza mchakato huu.
  • Kuundwa Tume ya Katiba
Tume ya kukusanya na kuratibu maoni ndicho chombo chenye dhima ya kushughulikia sehemu kubwa ya mchakato wa katiba mpya.  Chombo hiki chenye wajumbe 30, Mwenyekiti na Makamu wake, kimeundwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano kwa kushirikiana na rais wa Zanzibar April 6, 2012. Hatua hii imetanguliwa na ile ya bunge la Jamhuri ya Muungano kupitisha sheria ya mabadiliko ya katiba The Constitutional Review Act iliyopitishwa Novemba 18, 2011.
Tume ya Katiba itakuwa na sekretarieti yake ambayo ndiyo itakuwa mtekelezaji wa shughuli mbali mbali za tume kiufundi.
  • Ukusanyaji maoni kutoka kwa Wananchi
Tume itaendesha mikutano (mabaraza) ya hadhara ya ndani na nje, na hata kupokea maoni kwa njia ya maandishi kwa nchi nzima. Hii ndio kazi ya msingi ya tume mara baada ya kuundwa na kuapishwa wajumbe wake na Rais wa Jamhuri ya Muungano. Baada ya kazi ya kukusanya maoni Tume itaandaa rasimu ya katiba mpya itakayotokana na maoni iliyoyakusanya.
  • Rasimu ya Katiba mpya
Baada ya kukusanya maoni na kuandaa rasimu ya Katiba mpya iliyotokana na maoni yaliyotolewa, rasimu ya katiba mpya itachapishwa katika vyombo vya habari ili kutoa fursa kwa wananchi kuthibitisha maoni yao. Baada ya hatua hiyo rasimu ya katiba mpya itakabidhiwa kwa Rais wa Muungano na Rais wa Zanzibar.
  • Rasimu ya katiba mpya kujadiliwa na bunge maalum la katiba
Baada ya Rais kuipitia rasimu ndani ya siku 21 tangu akabidhiwe atatangaza Bunge Maalum la katiba. Bunge hili litaundwa na wajumbe wafuatao:-
  1.  Wabunge wote wa muungano
  2.  Wajumbe wa baraza la wawakilishi Zanzibar na
  3.  Wajumbe 166 kutoka:-
(a) vyama vya siasa vyenye usajili wa kudumu
(b) Asasi za kijamii(NGO’s)
(c) Jumuiya za Dini
(d)  Makundi ya wakulima
(e) Wafugaji.
(f) Taasisi za elimu ya juu
(g) Wafanyakazi
(h) Makundi mengine yenye maslahi ya pamoja
(i) Makundi yenye mahitaji maalum
Mwenyekiti wa Tume ya katiba atasoma rasimu hiyo kwa mara ya kwanza ndani ya bunge maalum la katiba na kukabidhi jukumu hilo kwa Mwenyekiti wa bunge la katiba ili ijadiliwe na bunge hilo na hatimaye kuipitisha au kuirejesha ikafanyiwe marekebisho. Endapo Bunge maalum la katiba litaipitisha rasimu ya katiba hatua itakayofuata ni kupigiwa kura ya maoni na watanzania wote.
  • Kura ya maoni
Baada ya rasimu ya katiba kupitishwa na bunge la katiba itakuwa katiba iliyopendekezwa na itakabidhiwa kwa Tume ya Taifa ya uchaguzi yaani NEC na Tume ya uchaguzi Zanzibar ZEC kwa ajili ya kuandaa na kusimamia kura ya maoni, kwa kupiga kura ya NDIYO au HAPANA. Ikiwa rasimu hiyo itakubaliwa na wananchi wa bara kwa 50% na visiwani kwa 50%, katiba mpya itakuwa imeundwa, na kwa matarajio ya serikali katiba hiyo itaanza kutumika Aprili 26, 2014.
7. KWA NINI WAISLAMU WANASHIRIKI KATIKA MCHAKATO WA KATIBA
Sababu kubwa ni Wajibu wa waislamu kupigania haki ili kuwa na katiba nzuri inayolinda haki zetu. Kuwa na katiba inayolinda haki za waislamu kama sehemu ya watanzania ni njia bora zaidi ya hakikisho la haki katika mfumo wa uendeshaji wa nchi kama hii inayojiita ya kisekula.
Kwa mfano katika Katiba iliyopo imechangia kwa kiasi kikubwa kuwaathiri Waislamu kiimani, kiuchumi na kijamii. Waislamu tumekosa haki ya kuwa na muwakilishi bungeni, haki ya kuwa na mfumo wetu wa elimu, haki ya kunufaika kwa misaada ya shirika la kimataifa la waislamu OIC, haki ya usawa katika miliki ya ardhi, haki ya usawa katika uteuzi wa ngazi mablimbali za uongozi wa nchi, haki ya kuheshimiwa sheria za kiislamu n.k.
Kutokana na udhaifu wa kikatiba serikali  kupitia amri ya Rais ilizifuta Mahakama za Kadhi mwaka 1963 na ilipofika mwaka 1971 bunge lilipitisha sheria ya ndoa. Sheria hii inazidhalilisha sheria za Kiislamu kwa kuhukumiwa na mahakama zisizo za kiislamu na pia kusimamiwa au kutafsiriwa na wasioziamini (wasiokuwa waislamu) na kusababisha kutolewa kwa tafsiri potofu.
Mwaka 1992 serikali iliingia mkataba wa maridhiano na Makanisa (MoU) kugharamia shughuli za kijamii, kiafya na kielimu za Wakristo bila ya kuwasikiliza waislamu au kutupa fursa kama hiyo sisi waislamu nk.
Aidha haki za msingi za raia wakiwemo waislamu hutolewa na kuhakikishiwa (guarantee) na katiba. Kwa katiba iliyopo sasa haki hizo hazipatikani kwa uwazi, uhakika na kwa haki; na endapo mtu au serikali ikivunja haki hizo ni vigumu mno kuchukua hatua kwa mfano tokea mauaji ya Mwembechai,1998 hakuna hatua yoyote iliyochukuliwa dhidi ya wauaji.
Kwa mantiki hiyo utaona wajibu wa kupigania mabadiliko ni MUHIMU SANA. Hofu yetu katika mchakato huu ni je, Tume ya katiba itafanya uadilifu kwa wananchi wote bila kujali dini? Hofu hiyo si kigezo cha kuturudisha nyuma na kuwaacha wasiokuwa waislamu kuyasemea yanayowahusu waislamu. Hivyo basi waislamu lazima tushiriki kuhakikisha uadilifu, haki vinazingatiwa, waislamu wanasikilizwa na maoni yao yanazingatiwa.
  • Uislamu na katiba
Mtume Muhammad (SWALALLAH ALAYHI WASALLAM) aliandika waraka wa makubaliano ya namna ya kuishi kati ya waislamu na jamii mchanganyiko alipofika Madina. Makubaliano haya kwa sasa yanaitwa katiba. Utaratibu huu ulimuwezesha Mtume (SWALALLAH ALAYHI WASALLAM) kujenga nguvu ya kusimamisha dola ya kiislamu ndani ya kipindi cha mpito.
  • Mtazamo wa Wanawazuoni wa Fiq-hi na mazingira yaliyopo
Waislamu kwa nyakati tofauti ima watakuwa wanaishi katika dola ya Kiislamu (Daarul Islaami) ama dola kama ya Tanzania ambayo si ya kiislamu. Katika dola ya Kiislamu, sheria zote za nchi chimbuko lake ni Allah (Subhaanahu Wataala), na katika dola isiyokuwa ya kiislamu ni kinyume chake. Waislamu tunaishi katika nchi hizi (Daarul harb) na katiba zake zinatuathiri sana kwa njia moja ama nyingine.
Kwa sababu hiyo tunalazimika kushiriki katika kuundwa kwake kwa lengo la kuondoa kabisa na ikibidi kupunguza madhara yake kwetu na kwa jamii na wala si kwa lengo la kuipa nguvu mifumo dhidi ya mwongozo wa Allah (Subhaanahu Wataala).
Hapana shaka Fatwa ya jumuhuri ya wanazuoni wa fiq-h na ile ya Kamati ya Kudumu ya Fataawa na Uchunguzi ya Saudia, Fatwa ya Al Azhar, Sheikh Al Uthayminyn, Ibn Jibriin, Nassur ad-Diyn Al-Albany n.k zilizopitisha kuwa inajuzu kwa waislamu kushiriki katika mambo mbalimbali (kama siasa, chaguzi nk) katika nchi za kitwaaghuti wanazoishi, zimezingatia hekma ya Qur’an na mafundisho ya Mtume (SWALALLAH ALAYHI WASALLAM).
  • Wajibu kwa viongozi wa Kiislamu
Kila jamii hutaraji maelekezo kutoka kwa viongozi wao. Kwa hiyo wajibu wa kwanza kwa kiongozi wa umma wa waislamu ni kujitambua kwamba waislamu wanamtegemea awaelekeze jinsi ya kushiriki kwa namna itakayoleta tija kwao na kwa taifa kwa ujumla.
Ili kutekeleza jukumu hili, kiongozi wa waislamu anapaswa kujifunza mambo muhimu kuhusu mchakato huu wa katiba, madai ya waislamu,  kura ya maoni na namna ya kutoa maoni kama kundi jamii.
Kiongozi pia anapaswa kuwa na ung’amuzi wa nini kinachoendelea katika kijiji, mtaa, mji, kata, tarafa, wilaya na Mkoa wake kuhusu mchakato wa katiba.
  • Wanataaluma wa Waislamu
Hawa ni wahasibu, wanasheria, wanasiasa, wachumi, walimu wa shule na vyuo, mabwana na mabibi afya, kilimo, mifugo, maafisa ardhi, wathamini, madaktari, wahandisi,wanafunzi (vyuo na sekondari) na huduma nyingine za jamii, wanategemewa sana kufafanua mambo ambayo wengine wasio na taaluma kama zao hawana namna ya kuyajua kwa namna yanavyoweza kuwanufaisha au kuwaathiri vibaya hususan yanapoingizwa ndani ya katiba. Wajibu wao mwingine ni sawa tu na ule wa viongozi wengine wa kiislamu kuanzia ngazi za msikiti, kijiji, mtaa, mji, kata, tarafa, wilaya na Mkoa.
  • Muislamu mmoja mmoja
Mbali na masheikh, wataalamu na viongozi wa kiislamu, kila muislamu anatakiwa awe macho na kufuatilia ratiba ya Tume ya Katiba ili ashiriki kutoa maoni. Aidha awe amejiandaa barabara kutoa maoni kwa kuelewa madai yetu ya msingi.
Muislamu mwanamke au mwanamme anao wajibu wa kuhakikisha elimu na ujumbe huu vinawafikia wengine ili waweze kushiriki kwenye mchakato wa katiba ili madai yetu yazingatiwe na kuingizwa kwenye katiba mpya.
Aidha kwa wale waislamu waliobahatika kuteuliwa katika Tume ya Katiba, na wale watakaochaguliwa katika bunge la katiba na kwa watakaopata fursa ya kutoa maoni, wanapaswa kuelewa kuwa  wanao wajibu mkubwa zaidi ya ule wa kitaifa. Yakiwezekana hayo tunaamini kwamba mchakato huu utakuwa na manufaa si tu kwa waislamu wa Tanzania bali wananchi wote ili kuitunza tunu ya amani ambayo Allah (Subhaanahu Wataala) ametutunukia watanzania.
  • Katika mchakato huu umakini wetu Unahitajika
Katiba ni chimbuko la mambo yote ya msingi kwa taifa na kimataifa. Kwa hiyo matakwa (maoni) halali ya wananchi hutolewa, hukusanywa na kuandikwa kwa mukhtasari mno ili mambo mengi ya msingi yapate nafasi ya kuingizwa ndani ya katiba.
Hivyo basi maoni yanapaswa kutolewa kwa mambo ya msingi. Kwa mfano, ni kweli tunataka vijana wetu wavae mavazi ya stara na tunakereheka sana wanapowaiga wahuni wa magharibi. Lakini hatuwezi kuiambia tume ya katiba kwamba “maoni yetu tunataka katiba itamke ni marufuku vijana kuvaa hereni au suruali chini ya makalio” na mfano wa haya. Maoni kama haya hayatozingatiwa kamwe kwa sababu kanuni na sheria juu ya mavazi zinapaswa kuwekwa na sheria zingine za bunge, Halmashauri za miji, Wilaya na Manispaa na si katika katiba ya nchi.
  1. MAMBO YA KUPIGANIWA NA WAISLAMU KATIKA KATIBA MPYA
Sehemu A. MASUALA YA MSINGI KWA WAISLAMU.
i. UWEPO WA MWENYEZI MUNGU
Hapa tunapendekeza Katiba mpya itambuwe uwepo wa Mwenyezi Mungu
Ibara ya 19 (1-3) inatoa uhuru wa imani na dini. Kwa kuwa katiba inatambua uwepo wa dini basi itambue pia uwepo wa Mwenyezi Mungu isipokuwa tu kwamba kila mtu awe huru kuamini Mungu kwa mujibu wa imani yake. Ikumbukwe kuwa viapo mbali mbali hutolewa mahakamani, bungeni na serikalini kwa wabunge, majaji, mahakimu, watendaji wa serikali n.k. Basi ni busara na uungwana Mungu huyo anayemuombwa kwa kusema “Ee Mungu nisaidie” uwepo wake utambuliwe katika katiba.
ii.  UBAGUZI WA KIDINI KWA SIKU ZA MAPUMZIKO UFUTWE.
Upendeleo wa kidini uondolewe. Mfano;- Siku za mapumziko Jumamosi na Jumapili ni siku za ibada kwa Wakristo. Hivyo ni vyema Ijumaa nayo iwe mapumziko walau nusu siku ili kuruhusu waislamu nao wawe huru kwa ibada hasa sala ya Ijumaa. Pia upendeleo wa  kidini katika pato la taifa uondolewe. Mifano mkataba wa Serikali na Makanisa maarufu  kama MoU unayoitaka serikali kutoa pato la taifa na kuipa dini hiyo huku dini nyingine zikinyimwa haifai. Katiba mpya ni vyema ikapiga marufuku suala kama hilo kutendwa na serikali.
iii. KATIBA ITAMBUE NA KUIREJESHA (REINSTATE) MAHAKAMA YA KADHI.
Katiba mpya itambue na iweke utaratibu wa uwepo wa Mahakama ya Kadhi ambayo itaendeshwa na waislamu wenyewe kama moja ya Mahakama za nchi. Mashauri yote yanayohusu ndoa, talaka, mirathi, waqf, malezi ya watoto, hibba (zawadi), wosia, biashara, bima kwa mujibu wa dini ya kiislamu yasikilizwe katika Mahakama ya Kadhi alimradi mhusika/wahusika ni waislamu.
Pawekwe kipengele kinachozuia rufaa za Mahakama ya Kadhi kwenda kwenye mahakama za kawaida.  Mahakama ya Kadhi iwe chombo chenye nguvu za dola na ipewe haki na uwezesahaji wa kifedha kutoka serikalini ili kutekeleza majukumu yake katika uendeshaji wa kesi.
Ni dhahiri kuwa baadhi ya sheria za kiislamu ni sheria
halali za nchi hii. Mfano sheria za ndoa na mirathi, sheria hizi hazipati tafsiri sahihi kutokana na mamlaka zilizopewa jukumu la kuzisimamia kuendeshwa kinyume na misingi ya dini ya kiislamu kwa asiyekuwa muislamu kuruhusiwa kutafsiri sheria za kiislamu.
hili pia linatokana na ujuzi finyu wa utambuzi matumizi ya hukmu za sheria hizi ambalo ni tatizo katika kusimamia haki zitokanazo na sheria za kiislamu. Kwetu sisi Waislamu kuhukumiwa kwa mujibu wa sheria za kiislamu ni tendo la kiibada na kijamii, na vile vile kuhukumiwa nje ya misingi hiyo ni matendo yanayoingilia uhuru wetu wa kuabudu.
Hivyo basi tunataka katiba mpya itambue na iweke utaratibu wa uwepo wa mahakama ya kadhi mahakama ambayo itaendeshwa kwa mujibu wa sheria za kiislamu katika mambo yahusuyo waislamu bila ya kuingiliwa na chombo chochote. Hakika hili ni eneo muhimu na nyeti sana kwa uislamu tunataka tume ya katiba isipuuze kwa namna yoyote hitajio hili kwa lengo la kulinda amani na kuheshimu imani na uhuru wa kuabudu kwa waislamu.
Ni pendekezo letu pia kuwa rufaa za mahakama ya kadhi zishughulikiwe bila ya kuhusisha mahakama za kawaida.
Tunataka mtu ambaye amefunga ndoa ya kiislamu au anaishi kama Muislamu na jamii inamtambua kuwa ni Muislamu iwe ni kigezo cha shauri lake la mirathi na ndoa kupelekwa katika Mahakama ya Kadhi na siyo ridhaa ya warithi au maoni ya mtu mwingine.
  1. iv.  ADHABU YA  KIFO KWA MUUAJI IENDELEE KUTAMBULIKA KIKATIBA
Yapo madai yanayotolewa kutaka adhabu ya kifo ifutwe kwa kuwa eti ni kinyume na haki za binadamu. Kuondolewa kwa adhabu ya kifo kutaleta hali ngumu kwa jamii na hasa wanyonge kwa sababu:-
  • Mauaji ya raia wasio na hatia yataongezeka sana.
  • Nchi zilizoondoa adhabu ya kifo kwa makosa ya mauaji, bado haikupunguza idadi ya wahalifu wa makosa ya mauaji. Mfano, Afrika ya kusini waliiondoa na sasa wanajadili kuirudisha.
  • Hoja ya wapinga adhabu ya kifo kuwa pamoja na adhabu hiyo kuwepo bado mauaji yanaendelea haina msingi kwani hata wizi na makosa mengine bado yapo japo wezi wanafungwa na magereza kupanuliwa kila siku. Je, ni busara kuondoa adhabu dhidi ya wezi kwa kuwa wezi bado wapo? Ni busara kuondoa adhabu dhidi ya makosa ya barabarani kwa kuwa ajali zinaongezeka?
  • Kosa la kuua linaumiza na linakwenda mbali sana zaidi ya kwa yule aliyeuliwa ndugu yake hivyo basi muuaji akiendelea kuishi kwa kulishwa na serikali kwa kodi za waliouliwa ndugu yao kutachochea mauaji na visasi zaidi, tunaamini salama yake nay a jamii ni muuaji naye kuhukumiwa kuuwawa kuzuia raia kujichukulia hatua mikononi mwao.

  • Hoja ya kwamba adhabu ya kifo haimpi muuaji nafasi ya kujirekebisha haina mantiki kwani adhabu si sehemu pekee ya kujirekebisha bali ni hukumu kwa matendo ya mtu na katazo (detterance) kwa wengine.

  • Pia hoja ya kwamba adhabu ya kifo inamdhalilisha mtuhumiwa nayo haina mantiki kwani hakuna adhabu ambayo inampa sifa mtuhumiwa; bali adhabu zote mfano kifungo, faini au viboko zinadhalilisha na ndio maana zikaitwa adhabu na sio pongezi.

  1. v.   KATIBA ITAMBUE HAKI YA WAISLAMU KUWA NA MFUMO WAO WA ELIMU

Nchi mbali mbali duniani zinaruhusu watu wa dini mbali mbali kuwa na mfumo wao wa elimu ili kutoa nafasi ya kufundisha watoto wao imani, mila na desturi zao alimradi wanaingiza na mitaala ya kiserikali. Afrika ya Kusini, Uingereza, India na hata Marekani hufanya hivyo.

Waislamu tumeruhusiwa kuanzisha mashule yetu lakini yanadhibitiwa mitaala, vitabu, kanuni na sheria mbali mbali na Wizara ya Elimu kiasi kwamba sisi ni waathirika wakubwa wa kufutiwa mitihani, kuhujumiwa hujuma mbali mbali pamoja na watoto wetu kuzuiwa kutekeleza dini yao katika shule na vyuo vya serikali. Mfano, sakata la wanafunzi wa Kiislamu ndanda Mkoani Mtwara kufukuzwa shule kwa kutekeleza uislamu wao.

Katiba itamke wazi kuwa wananchi wana uhuru wa kuwa na mfumo wao wa elimu kwa mujibu wa dini yao. Tayari kuna shule na vyuo (Akademia) vinavyoendeshwa kwa mitaala ya Uingereza na hata Marekani hapa nchini kwa nini isiruhusiwe waislamu kuendesha shule na vyuo kwa mitaala yao kama ilivyo kwa Vyuo vyao Vikuu? Kuendelea kulazimisha mfumo wa elimu wa pamoja ni kukiuka misingi ya haki za binadamu na uhuru wa mawazo (freedom of opinion).

Sehemu B.  HAKI ZA MSINGI ZA BINADAMU

HAKI YA UHURU KAMILI WA IBADA NA UWAKILISHI KIDINI.

a)   Katiba itoe haki na uhuru kamili wa kuabudu

Katiba ya sasa inatoa uhuru wa kuamini na uchaguzi katika mambo ya dini (Ibara 19: 1-3) lakini haitoi uhuru wa kuabudu. Hii inafanya baadhi ya waumini kulalamika kwamba hawapati uhuru kamili wa kuabudu. Baadhi ya masuala yanayolalamikiwa ni pamoja na ya akina mama wa kiislamu jeshini, polisi, na baadhi ya ofisi kutoruhusiwa kuvaa hijab, wanazuiliwa kuswali katika mashule, vyuoni na maeneo ya serikali nk.

Katika uhuru wa ibada, sheria za kiislamu ziheshimiwe mfano mirathi, ndoa, talaka, waqf, biashara, bima n.k. zitambuliwe kikatiba kama sehemu ya ibada yetu. Hii itafanya Mahakama ya Kadhi iwe na maana kwani sheria zitakazotumika katika mahakama hizo zitakuwa zinatambuliwa na hivyo haitakuwa rahisi kuziondoa kama ilivyopata kutokea huko nyuma.

Hili linajitokeza pale ibada hizi muhimu zinakandamizwa kwa vigezo vya haki za binadamu vya kimagharibi bila kuzingatia kwamba haki ya kuwa katika dini ni ya hiyari na kwamba mtu anaingia na kubaki katika dini akijua iko hivyo.

b)   UWAKILISHI WA KIDINI BUNGENI

Katiba itamke uwepo wa viti maalum vya uwakilisha wa makundi ya dini hasa Waislamu na wakristo Bungeni. Bunge ndio mhimili wa dola unaowakilisha maoni na matakwa ya wananchi. Hali ilivyo hivi sasa yanapojitokeza mambo yanayowahusu waislamu na wanadini wengine bungeni maoni yao hayapati nafasi wala kuzingatiwa.

C )  TUNATAKA UWAKILISHI WA KIDINI KATIKA BARAZA LA MADIWANI

Katiba itamke kama tulivyopendekeza katika uwakilishi wa Waislamu na wakristo bungeni kwamba katika serikali za mitaa pia kuwe na uwakilishi kama huo.

d)   SHERIA YA UGAIDI IFUTWE

Katiba mpya ipige marufuku sheria ya ugaidi ya mwaka 2002 na utungwaji wa sheria kama hizo zinazopelekea kuvunjwa kwa haki za msingi za binadamu na ambazo utekelezaji wake unaleta manyanyaso na madhara makubwa kwa Waislamu kama ilivyo sasa Tanzania.

e)   Haki za Binadamu ziendane na Maadili ya Dini na ya Kitanzania

Tunataka katiba mpya isiruhusu mambo ya kishetani kama vile ulawiti, ndoa za jinsia moja, utoaji wa mimba, uhuru wa kupindukia wa mtoto dhidi ya wazazi wake na mfano wa hayo kuwa ni miongoni mwa haki za binadamu. Zipo kampeni zinazoshinikizwa na makundi yanayojiita watetezi wa haki za binadamu na hata baadhi ya nchi za nje kama vile Uingereza kutaka kushinikiza kuingizwa mambo hayo katika katiba mpya.

f)   Katiba Mpya itoe ainisho sahihi la ndoa na familia

Kutokana na shinikizo la ushoga dhidi ya nchi yetu ni muhimu katiba itamke wazi maana ya ndoa. Katiba itamke hivi ‘ndoa ni baina ya mwanaume na wanawake au mwanaume na mwanamke.

Ndoa kati ya watu wa jisnia moja zisiruhusiwe na iwe ni kosa la jinai iwapo watu wa jinsia moja watabainika kuoana au kuishi kama mke na mume ili kulinda maadili yetu.

g)   Nafasi mbali mbali za uteuzi serikalini na mashirika ya umma zizingatie uwiano
     wa kidini kati ya Wakristo na Waislamu.

Katiba mpya iweke utaratibu kuwa nafasi zote za uteuzi serikalini na katika idara zake, uwakala wa asasi za serikali nk zizingatie uwiano ulio sawa baina ya dini za waislamu na wakristo, ili kuondoa manung’uniko kuwa kuna ubaguzi katika uteuzi wa nafasi za uongozi serikalini.

Hii itasaidia kuweka misingi ya usawa katika utumishi wa umma na kuondoa hisia za udini. Salama ya nchi hii kwa kiasi kikubwa inategemea kuaminiana na kuheshimiana baina ya dini hizi kuu mbili, hivyo basi uwiano katika uteuzi ukilindwa kikatiba itakuwa ni kujenga msingi imara wa amani, haki na kuaminiana.

h)   Urekebishwaji wa vifungu vya haki za binadamu ndani ya katiba

Pia tunapendekeza kuwepo taratibu makhsusi za urekebishaji wa vifungu vya haki za binaadamu katika Katiba. Utaratibu wa sasa wa vifungu hivyo kurekebishwa kama vifungu vingine vya Katiba ni hatari kwa kuzingatia umuhimu na unyeti wa haki za binaadamu katika maisha yetu.

Vifungu kama vile vinavyohusiana na haki ya kuishi, kuchagua na kuchaguliwa, kuabudu, kufanya kazi, kutokubaguliwa, uraia na kumiliki mali visibadilishwe mpaka iwepo ridhaa ya wananchi kwa njia ya kura (referendum).

Haki nyingine za Katiba zisibadilishwe mpaka zaidi ya asilimia 75 ya wabunge kutoka pande zote za Muungano waridhie na pia iwepo haki ya wananchi wasioridhika na mabadiliko hayo  kuyapinga katika Mahakama Kuu ya Katiba ndani ya siku tisini toka marekebisho hayo yalipofanyika.

Muswada wowote wa kurekebisha kifungu chochote kinachohusu haki za Binaadamu lazima usambazwe kwa wananchi kutoa maoni yao ndani ya siku 90 kabla haujasomwa Bungeni na kisha upigiwe kura ya maoni.

Ili kulindwa kwa haki za kibinadamu na kuwepo kwa uwazi tunapendekeza sheria zote kandamizi maarufu kama sheria 40 zilizoorodheshwa na tume ya jaji Nyarali zifutwe.

Adhabu ya kifo kwa makosa makubwa kama mauwaji ya makusudi iwepo katika katiba mpya na iwe ni moja kati ya mambo ambayo hayawezi kubadilishwa bila referandamu (kura ya maoni).

i)   Mahakama Kuu ya Katiba na haki za binadamu

Tunataka katiba mpya iruhusu uwepo wa Mahakama Kuu ya Katiba ambayo itapewa uwezo na nguvu za kisheria wa kutafsiri vipengele mbali mbali vya katiba na pia kubatilisha sheria yoyote itakayotungwa ambayo inapingana na katiba.
Mahakama hii pia izuie marekebisho ya Katiba yanayokinzana na misingi ya Katiba yenyewe. Na ili hili liwe na mantiki, Katiba itamke wazi kwamba baadhi ya vifungu vya Katiba kama vile vinavyohusu Muundo wa Dola, Muungano, haki za binadamu makhsusi zinazorekebishika kwa ridhaa ya wananchi ndio utakuwa msingi mkuu wa katiba na kwamba haiwezi kubadilishwa bila kuwa na ridhaa ya wananchi kupitia kura ya maoni (referendum).
Pawepo na Mahakama Kuu ya Katiba ambayo itakuwa na hadhi ya muungano na pia pawe na Mahakama ya Rufaa ya Katiba ambayo pia itakuwa ya muungano. Mahakama Kuu ya Tanganyika na Mahakama kuu ya Zanzibar kama ilivyo Mahakama ya Rufaa ya Tanganyika zisiwe sehemu ya Muungano.
j)   Mahakama za hakimu mkazi
Mahakama za Hakimu Mkazi zifutwe na badala yake ziwepo Mahakama za Wilaya ambazo zitaendeshwa na Mahakimu wa Daraja la Pili ambao watakuwa na uzoefu wa kuwa mahakimu wa mahakama za mwanzo kwa kipindi kisichopungua miaka mitano.
Mfumo wa sasa hivi wa kuwa na mahakama za wilaya na mahakama za hakimu mkazi ambazo zinakaribu mamlaka sawa hauna tija. Na pia mfumo wa kuwapa uhakimu mkazi wahitimu wa chuo wasiokuwa na uzoefu wowote unakwaza utoaji haki. Ni bora mahakimukama hao wakaanzia mahakama za mwanzo.
k) Haki ya kumiliki Ardhi
Haki ya kumiliki Ardhi iwe ni haki ya raia. Mgeni anaweza kuruhusiwa kumiliki ardhi kwa kushirikiana na mzawa tu na kwa masharti kwamba hamiliki zaidi ya asilimia 45 ya ardhi hiyo ya pamoja na kwamba umiliki wake uwe ni kwa ajili ya uwekezaji na si makazi.
Pawepo na ukubwa maalumu wa ardhi mtu mmoja atakubaliwa kumiliki. Zaidi ya hapo raia awe na haki ya kukodisha ardhi anayoimiliki kwa muda usiozidi miaka kumi na tano. Hii inakusudia kuondoa uwezekano wa mtu mmoja au kikundi cha watu kumiliki na kuhodhi eneo kubwa la ardhi na kuacha jamii kubwa ya watanzania wakikosa haki ya kumiliki ardhi. Ikumbukwe kuwa ardhi haiongezeki bali watu wanaongezeka.
Mamlaka ya Raisi ya kutwaa ardhi kwa maslahi ya umma iweke wazi mambo yanayohesabika ni maslahi ya umma na itoe muda maalum kwa mtu asiyeridhika kukata rufaa dhidi ya uamuzi wa kutwaliwa ardhi yake katika Mahakama ya Ardhi .
Katiba ielekeze Sheria za mipango miji zitenge maeneo ya dini (ibada) kwa kuainisha maeneo ya waislamu, wakristo na dini zingine kama vile majumba ya ibada, makaburi n.k. na sio kutaja kiujumlajumla “eneo la kidini” kama ilivyo sasa.
Kitendo cha kutaja kiujumlajumla “Eneo la Kidini” bila kuainisha dini gani kinafanya makundi ya dini moja kuhodhi maeneo makubwa kuliko makundi mengine na hivyo kusababisha manung’uniko.
Sehemu C.  MUUNDO WA SERIKALI NA MUUNGANO

i.   Tunapendekeza nchi yetu iwe na serikali tatu, yaani serikali ya Muungano, serikali ya Tanganyika na serikali ya Zanzibar

Pendekezo hili linalenga kuturejesha katika dhamira ya uasisi wa Muungano kama unavyojidhihirisha katika hati ya Muungano ya 1964 ambao ulibainisha wazi kuwepo kwa muungano wa nchi mbili na serikali tatu. Hili pia linalenga kuondoa malalamiko ya mara kwa mara ya kila upande kuona unaburuzwa au kuonewa ndani ya mfumo wa serikali mbili tulionao hivi sasa. Vile vile litatibu kilio cha Wazanzibari kujiamulia mambo yao na kile cha watanganyika kufutiwa serikali yao.

Mfumo wa sasa wa himaya tatu katika serikali mbili una matatizo mengi kiutendaji na kisiasa hasa katika himaya ya Tanganyika ndani ya serikali ya Jamhuri. Kwa mfano, nafasi kama ya Waziri Mkuu, Mwanashera Mkuu wa Serikali zinazua utata kama ni nafasi za muungano au Tanganyika. Maana, hadhi ya Waziri Mkuu haitambuliki Zanzibar na kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali Zanzibar nako kuna Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

Pia wabunge wa Zanzibar katika Bunge la Jamhuri ya Muungano chini ya mfumo huu wanapata nafasi ya kujadili na kutoa maamuzi juu ya masuala ya Wizara za Tanzania Bara kama vile Wizara ya Elimu wakati wabunge wa Tanzania Bara hawana nafasi hiyo katika Wizara za Zanzibar.

ii.  Tunapendekeza Urais wa serikali ya muungano uwe ni wa kupokezana kwa Tanganyika na Zanzibar

Ili kuondoa manung’uniko kama tulivyoeleza hapo juu sisi waislamu tunaona kwamba umefika wakati sasa nafasi ya uongozi wa Rais wa Serikali ya Muungano iwe ni ya kupokezana. Tunataka utaratibu huo sasa uwe rasmi kikatiba.


iii. Mambo yaliongezwa katika orodha ya mambo ya Muungano yaliyopo katika hati ya Muungano yajadiliwe upya 

Masuala yatakayokubalika kuwa ya Muungano yasirekebishwe isipokuwa kwa  ridhaa ya wananchi wa sehemu zote za Muungano kwa njia ya kura ya maoni (referéndum). Ili kulinda maslahi ya Zanzibar kutokana na idadi yao, kura  zitazingatia uwiano wa sehemu mbili za Muungano na sio idadi ya watu.

Katika masuala yanayoweza kukubalika kama masuala ya Muungano, Katiba ya Jamhuri ya Muungano na Katiba za Tanganyika na Zanzibar zitamke bayana kwamba iwapo kutakuwa na ukinzani wowote kati ya Katiba ya Jamhuri na Katiba za Zanzibar na Tanganyika kuhusiana na masuala ya Muungano, katiba za nchi hizi zitakuwa batili kwa kiwango cha ukinzani kwenye vifungu husika. Hili litalinda uwezekanao wa kuwepo migogoro inayotokana na moja kati ya nchi hizi kurekebisha katiba kwa namna inayoweza kuvuruga sura ya Muungano. Mabadiliko ya Katiba ya Zanzibar ya hivi karibuni yanaweza kutoa picha ya uwezekano huu.

iv.  MAHAKAMA NA MUUNGANO

Kwa maoni yetu, isipokuwa tu kwa masuala yanayohusu tafsiri ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano, Mahakama ibaki kuwa suala lisilo la Muungano. Ili kuweka mfumo mzuri wa utatuzi wa migogoro ya Katiba, iwepo Mahakama Kuu ya Katiba ambayo itakuwa na hadhi ya Muungano bila kujali kama ipo Zanzibar au Tanganyika. Pia iwepo Mahakama ya Rufaa ya Katiba ambayo itasikiliza Rufaa kutokana na maamuzi ya Mahakama Kuu ya Katiba. Mahakama Kuu ya Rufaa ya Katiba pia iwe na uwezo wa kusikiliza Rufaa toka Mahakama Kuu za Tanganyika na Zanzibar kwa maamuzi yanayohusiana na tafsiri ya Katiba za Zanzibar na Tanganyika.

v. MALIASILI NA MUUNGANO

Kwa maoni yetu masuala ya madini na mafuta hayana sababu yoyote ya kuwa masuala ya Muungano. Ni bora yakabaki katika serikali husika ili kuondoa malalamiko kwamba sehemu moja ya muungano inataka kujinufaisha na maliasili zilizopo katika sehemu nyingine.

vi)  URAIS WA TANGANYIKA

Tunapendekeza kwamba Uraisi wa Tanganyika uwe wa kupokezana kuzingatia makundi makubwa ya kijamii waislamu na wakristo. Kwa muda mrefu katika serikali ya Tanzania, hasa katika kipindi cha mfumo wa chama kimoja, kumekuwa na  kanuni, japo hazikuandikwa, za kupokezana uraisi kati ya waislamu na wakristo. Utaona kwamba Raisi wa kwanza alikuwa mkristo, akarithiwa na Raisi wa Pili Mwinyi ambaye ni muislamu. Mwinyi akarithiwa na Mkapa ambaye ni mkristo naye akarithiwa na Kikwete ambaye ni muislamu.

Kwa mazingira yetu ambayo uwiano wa idadi kubwa ya watanzania ni aidha waislamu ama wakristo na ukizingatia mvutano wa chini chini unaojitokeza kati ya wanadini hizi kuu mbili nchini kuhusiana na uwakilishi katika dola, ni busara kama mfumo huu aliotuachia mwalimu ukaendelezwa na ikibidi kulindwa  kikatiba. Mfumo huu pia unaweza kuwa msingi wa kulinda umoja wetu na uvumilivu.

vii. BARAZA LA MAWAZIRI NA UBUNGE

Tunapendekeza Baraza la Mawaziri lisitokane na wabunge kama ilivyo sasa. Hii inatokana na ukweli kuwa mara kwa mara kumetokea mgongano wa kimaslahi kwa mawaziri kupeleka miradi mingi ya maendeleo katika majimbo yao ili kujijengea uhalali wa kuchaguliwa tena. Vile vile pendekezo hili linalenga kutenganisha utendaji wa mihimili miwili ya serikali na bunge. Haileti maana nzuri wabunge kuwa sehemu ya serikali  (executive) kwani ile dhana ya mgawanyo wa madaraka ambayo ni muhimu katika kuhakikisha utendaji na ufanisi haionekani kuleta tija inayotegemewa katika mfumo huu tulionao wa mawaziri kuwa sehemu ya bunge.

viii. SPIKA WA BUNGE LA JAMHURI YA MUUNGANO

Ili kutoa nafasi sawa katika pande zote za Muungano, ni bora nafasi ya  Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iwe ya kupokezana kati ya Tanganyika na Zanzíbar.

Aidha iwapo Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano atatoka upande mmoja wa Muungano basi naibu wake atoke upande wa pili. Katibu wa bunge pia iwapo atatoka upande mmoja wa Muungano naibu wake atoke upande wa pili wa Muungano.

ix.SPIKA WA BUNGE LA TANGANYIKA

Katika serikali ya Tanganyika kwa yale mambo ambayo si ya muungano tunapendekeza bunge la Tanganyika liwe na spika wake kwa kuzingatia uwiano kama tulivyopendekeza kwa nafasi ya urais wa Tanganyika au uwepo utaratibu mwingine maalum unaofanana na huo.

Nafasi ya katibu wa bunge pia iwe kama katibu ni wa dini moja basi naibu wake awe kutoka dini nyingine.

x.   WIZARA ZA SERIKALI

Ili kuleta ufanisi na kumpunguzia Raisi majukumu na madaraka, ni bora muundo na idadi ya Wizara zikatamkwa moja kwa moja ndani ya Katiba badala ya utaratibu wa sasa wa wizara na idadi yake kutegemea matashi ya Raisi.

xi.  MAKAMU WA RAISI

Tungependekeza kama serikali ya Tanganyika itakuwepo, nafasi ya Makamu wa Raisi wa Tanganyika isiwepo na badala yake pawepo na Raisi na Waziri Mkuu tu. Utaratibu wa sasa wa kuwa na mgombea mwenza ambaye anakuwa Makamu wa Raisi wa Jamhuri ya Muungano uondolewe na badala yake kama Raisi anatoka Zanzibar Raisi wa Tanganyika awe kwa nafasi yake  ni Makamu wa Raisi wa Jamhuri na kinyume chake.

Ingawa kuna uwezekano wa Raisi wa Muungano kutoka chama tofauti na chama cha Raisi wa upande wa muungano utakaostahili kutoa Makamu wa Raisi, mfumo huu ni mzuri na wa lazima maana utakuwa umelinda maslahi na uwakilishi wa watu wengi katika upande wa Muungano unaohusika. Hii pia itawezekana maana serikali ya Muungano itakuwa inahusika na masuala machache ya muungano wakati masuala mengi yakishughulikiwa na serikali zinazounda muungano.

xii. MANAIBU WAZIRI
Tungependekeza pia nafasi ya Naibu Waziri kwa upande wa serikali ya Tanganyika isiwepo maana inaongeza gharama bila sababu.Katibu Mkuu wa wizara anatosha.

Kwa upande wa serikali ya Muungano, nafasi hiyo iwepo ili kuleta uwakilishi sawa kutoka pande mbili za muungano. Na pale Waziri akitoka upande mmoja wa muungano, naibu wake atoke upande wa pili wa muungano.

xiii. SERA RASMI YA NCHI

Tunapendekeza será ya nchi yetu iwe ni será ya kujenga ustawi wa jamii yaani “welfare state policy” badala ya será ya ujamaa ambayo kivitendo haipo tena. Pendekezo hili linazingatia ukweli kuwa sasa nchi yetu ni ya kibepari. Hivyo basi sisi waislamu tunaona kuwa ni heri sera ya nchi yetu iwe ni kuimarisha ustawi wa kijamii yaani ili kuifanya serikali iweze kuwajibika zaidi kwa wananchi kuwawekea ustawi wa maisha yao.


xiv. BAADHI YA MASHARTI YA KUSAJILI VYAMA VYA SIASA YAONDOLEWE

Kwa kuwa kila mtu ana uhuru wa kujiunga au kutojiunga na chama chochote cha siasa. Masharti yafuatayo ya uanzishwaji wa vyama vya siasa yaondolewe:-

  1. Sharti la kwamba chama cha siasa lazima kiwe na wanachama kwa Zanzibar na Bara liondolewe kwani linanyima uhuru na uchaguzi wa kujiunga na wengine kwa ridhaa ya mtu.

  1. Sharti la kuwa na wanachama mikoa 10 bara na 2 zanzibar liondolewe kwani halina mantiki. Chama kisicho na wanachama kiachwe kife chenyewe kwa kukosa wanachama.

  1. Vyama vya kidini viruhusiwe ili wananchi waamue wenyewe katika sanduku la kura. Hili linawezekana na kuna mifano hai kama vile Ujerumani, Australia,Uingereza, Canada,DRC Kongo,Denmark,Ufaransa,Italia, Rwanda, Ubelgiji, Afrika ya Kusini n.k na wala hakuna matatizo yoyote.


xv.  MAMLAKA YA RAISI YAPUNGUZWE

Japo mamlaka ya kutosha kwa Raisi ni muhimu kwa maslahi ya umma ili kumuwezesha kutekeleza majukumu yake makubwa kama Mkuu wa Nchi na Dola, ni bora, kwa lengo la utawala bora na kulinda zaidi maslahi ya umma, madaraka ya Raisi yakapunguzwa katika maeneo yafuatayo:-

. Raisi asiwe na mamlaka ya kuweka watu vizuizini bila ya kufikishwa mahakamani na
  Kuhukumiwa kwa kuthibitishwa shutuma dhidi yake.

. Mamlaka ya Raisi ya kusamehe wafungwa yawe ni kwa mujibu wa vigezo maalumu
vinavyotamkwa na sheria ya Bunge na iwe katika utaratibu ulio wazi.

. Mamlaka ya Raisi ya kuunda idara mbalimbali za serikali pamoja na kuteua
wakurugenzi yatumike kutokana na mapendekezo yatakayotolewa na Kamisheni ya Ajira
na Idara za Serikali itakayoundwa kutokana na uwiano wa kimakundi ya kijamii.

xvi. VYOMBO VYA UTEKELEZAJI WA SHERIA, UPELELEZI NA UENDESHAJI WA MASHITAKA

a)   Mkurugenzi wa mashtaka

Mamlaka ya Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) yanahitaji kupunguzwa ili kuleta ufanisi na uwazi zaidi katika mfumo wa utekelezaji wa sheria. Kwa maoni yetu, pale kesi ya jinai itakapoanzishwa na taasisi nyingine au mtu binafsi, DPP asiwe na uwezo wa kuidhinisha kesi hiyo kwenda au kutokwenda mahakamani, kuondoa mashitaka mahakamani wala kuingilia isipokuwa tu kama atatoa sababu za kisheria zitakazomridhisha hakimu au Jaji anayesikiliza kesi kwamba kuna mwenendo unaoweza kupelekea haki kutokutendeka.

Katiba na sheria tulizonazo kwa sasa zimetoa mamlaka makubwa sana kwa Mkurugenzi wa Mashitaka, kwani kwa mamlaka aliyonayo anao uwezo wa kuingilia au kuifuta kesi yoyote iliyo mahakamani bila ya kulazimika kutoa sababu yoyote na hakuna atakayemzuia kufanya hivyo. Hii imeleta maswali na malalamiko mengi kuwa wapo watu wanaofaidika na mamlaka hayo makubwa ya DPP kutoweza kufikishwa Mahakamani kwa matendo yao.

b)   Taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa PCCB

Tunapendekeza ofisi ya Kikosi cha Kuzuia na Kuondoa Rushwa Tanzania (PCCB) itamkwe ndani ya Katiba na iwe na mamlaka kamili na huru katika kusimamia sheria ya kuzuia rushwa bila kuingiliwa na ofisi ya DPP. Utaratibu wa sasa wa baadhi ya makosa kuhitaji ridhaa ya DPP kabla ya kupelekwa Mahakani yanaleta matatizo kiutekelezaji na yanapunguza uhuru wa PCCB.

Ni bora pia, ili kuondoa muingiliano, sheria ya PCCB ijihusishe na makosa makhsusi ambayo hayatamkwi katika Sheria ya Makosa ya Jinai (Penal Code). Na lau baadhi ya makosa katika Penal Code yanastahili kuwemo katika sheria ya PCCB, sheria ya Penal Code irekebishwe kuyahamishia makosa hayo katika sheria ya PCCB.

c) Ofisi ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa serikali (CAG)

Ili kuzuia ubadhilifu wa mali za umma ni bora ofisi ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa hesabu za Serikali iwe na uwezo wa kutoa ushauri kwa mamlaka zinazohusika na mashitaka ya kushitakiwa au kumfungulia mashitaka yeyote atakayeonekana kuwa na makosa kwenye taarifa ya hesabu za serikali. Na endapo vyombo husika vitakataa ushauri bila kuwa na sababu ya msingi kwa mtizamo wa Mkaguzi Mkuu, Sheria impe nguvu kulipeleka suala Mahakama Kuu ili iamue kama kuna haja ya kesi hiyo kufunguliwa.

d)   Tume ya Taifa ya Uchaguzi

Tunapendekeza utaratibu wa sasa wa Raisi kuunda Tume  ya Uchaguzi ubadilishwe badala yakeiundwe na Chombo cha Kikatiba kitakachokuwa katika muundo unaozingatia uwiano wa maslahi ya kisiasa na kijamii.  Hili litaondoa malalamiko kwamba Raisi anaunda Tume ya Uchaguzi kwa kuzingatia maslahi ya chama chake.

e)   Muundo wa Tume ya Uchaguzi uwe wa kitaifa kuanzia chini hadi juu

Muundo wa tume kipande unawafanya viongozi wa Serikali wa Kuteuliwa na Raisi kuwa watendaji wa misimu wa Tume na hivyo kuzua malalamiko mengi kwamba haifanyi kazi kwa uhuru.

f)   Matokeo ya Kura za Urais

Katiba iruhusu matokeo ya Uchaguzi wa Raisi kupingwa katika Mahakama Kuu ya Katiba. Ili kulinda usalama wa nchi kesi hiyo itapaswa kufunguliwa ndani ya siku kumi na tano toka matokeo yalipotangazwa na kusikilizwa ndani ya siku thelathini.

Mara baada ya kesi hiyo kufunguliwa, Katiba itamke kwamba Raisi aliyemaliza muda wake atakaimu nafasi ya Raisi ili kutoa nafasi kesi kusikilizwa kwa uhuru. Pia Katiba itamke wazi kwamba, kabla kesi hiyo haijafunguliwa, Mahakama Kuu ya Katiba itafanya upembuzi wa ushahidi uliopo kuona kama kuna sababu zozote za msingi za kufunguliwa kwa kesi. Utaratibu wa sasa wa matokeo ya Raisi yanayotangazwa na tume kuwa uamuzi wa mwisho hata kama kuna malalamiko ya msingi yanazua wasiwasi kuwa haki haitendeki.

g)   Mgombea Binafsi.

Mgombea binafsi aruhusiwe katika nafasi zote isipokuwa nafasi ya Raisi. Mfumo wa sasa unaolazimisha mgombea kuwa na chama cha siasa unawanyima wananchi wasio na vyama vya siasa kushiriki katika uongozi wa nchi kwa kutumia haki yao ya kuchagua na kuchaguliwa.
Kwa upande wa Raisi, mantiki ya kutaka wagombea wawe na vyama vya siasa ni kutoa nafasi ya kutosha kwa wananchi kutathimini sera vyama vyenye mgombea Urais ambazo ndizo zitakazotekelezwa na serikali itakayoundwa na Rais atakayeshinda. Na pia kutoa nafasi kwa Tume ya Uchaguzi kutathimini sifa ya mgombea. Yawezekana mtu akajitokeza kuwa mgombea Uraisi na akawa na Sera inayopingana na Katiba na maadili ya nchi. Kuwa na chama cha siasa kutaifanya Tume kuchukulia kwamba sera za mgombea ni kama zilivyo katika Katiba na Sera ya chama chake.

h)   Mfumo wa serikali za Majimbo urejeshwe

Katiba isiwe na nafasi za Mkuu wa Mkoa, Wilaya na badala yake kuwe na uongozi wa majimbo na viongozi wa majimbo hayo watoke katika majimbo hayo na wapigiwe kura na wananchi wa majimbo husika.

i)   Uhusiano na Jumuiya za Kimataifa Usiwe wa Kibaguzi

Katiba itamke kuwa Tanzania inaweza kujiunga au kuwa na uhusiano wa kibalozi, uanachama au vinginevyo na jumuiya yoyote ya kimataifa pasina kujali kama jumuiya hiyo ni ya kisiasa, kiuchumi, kijamii au za kidini alimradi kufanya hivyo itathibitika kuwa na maslahi kwa watanzania au sehemu ya watanzania.

Ni kwa msingi huu waislamu wa Tanzania tunataka Tanzania ijiunge na OIC kama ambavyo ina uhusiano wa kibalozi na Papa ambaye ni kiongozi wa Dola ya Kidini ya Vatican ya Kanisa Katoliki.Kama hili la kujiunga na OIC haliwezekani, basi iwe pia Ubalozi wa Vatican nchini Tanzania usiwepo kwa sababu ni ubaguzi wa kidini.

j)   Mali za viongozi zihakikiwe kabla na baada ya kutoa madarakani.

Katiba iweke utaratibu maalum kwa mali za viongozi kuhakikiwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa serikali (CAG) wakati wa kuingia madarakani na wakati wa kutoka badala ya Tume ya Maadili ya Viongozi.

Hii ni kutokana na ukweli kwamba wajumbe wa Tume ya Maadili wengi wao wanaweza wasiwe na ujuzi wa kutathmini na kuhakiki mali hivyo atumike CAG. Na iwe ni kosa la kisheria kukaidi utaratibu huo.

k)   Rasilimali za maeneo husika ziwanufaishe wenyeji wa maeneo husika

Katiba itamke kiwango ambacho wananchi wa maeneo yenye rasilimali kama vile gesi, madini n.k wanatakiwa wapatiwe kutoka kwa muwekezaji ili kuzuia kuhamisha mali kutoka eneo hilo kwenda kwingine au hata nje ya nchi bila wenyeji kunufaika.

l)   Muungano wa Tanganyika na Zanzibar uwe wa Mkataba

Katiba itamke kuwepo kwa Muungano wa mkataba na mambo yote ya Muungano yaliyoongezwa kutoka kwenye mkataba wa awali wa mwaka 1964 yapitiwe upya na pande zote husika.

HITIMISHO

Ndugu muislamu hii ni sehemu tu ya yale ya msingi kwa waislamu; yako mengine ambayo yanaweza kuongezwa wakati wa utoaji wa maoni, tafadhali muislamu uwe huru kuyatoa mbele ya tume alimuradi hayapingani na maoni yetu ya msingi, vinginevyo pata ushauri zaidi toka kwa jukwaa la katiba la waislamu JUWAKATA:-
 Simu ya M/Kiti wa Jukwaa – 0785 955 859/0715955859
Simu ya Makamu M/Kiti wa Jukwaa -0784863539
Simu ya M/Kiti wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Tanzania- 0689378747
Simu ya Makamu Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu – 0715631183
Sisi waislamu hatupaswi kutofautiana katika mambo ya msingi kwa ajili ya dini yetu. Tupo wanachama wa vyama mbalimbali vya siasa, lakini tukiingia msikitini imamu wetu ni mmoja, hii ni fundisho kuwa sisi ni ummah mmoja. Tetea itikadi yako ya kisiasa alimuradi haipingani na dini yako. Itikadi ya kisiasa haipaswi kwenda kinyume na uislamu wako. Tafadhali jitambue na uutambue uislamu wako na uwe tayari kuutetea popote.
Baada ya maelekezo haya, tunamuomba kila muislamu sasa kujifunga kibwebwe na kusimama kutekeleza jukumu lake kwa uwezo wake wote. Nia zetu ni njema katika kushiriki mchakato wa mabadiliko ya katiba Tanzania na Allah (Subhaanahu Wataala)ni shahidi wa nia zetu. Tunashiriki ili kuona kwamba katiba inazingatia matakwa yetu na ya wengine yasiyo na madhara kwetu na haitoi nafasi ya mtu yoyote kunyanyaswa.
Ni wazi tutakapo simama na kudai haya tuliyoyasema tutasikia mengi kutoka kwa wale wote wasioutakia mema Uislamu na waislamu. Wajibu wako wewe Muislamu kuitetea dini yako kwani kuna ujira mkubwa kesho mbele ya Allah (SW). Hautokuwa na udhuru wowote utakaposhindwa kusimama kuutetea uislamu ili hali umepewa nafasi ya kuutetea uislamu wako kupitia mabadiliko ya katiba.
Tumedhulimiwa kiasi cha kutosha ni wajibu wetu sasa TUSEME TUMECHOSHWA KUDHULUMIWA, TUNATAKA HAKI ZETU NDANI YA KATIBA MPYA.
TAFADHALI TIMIZA WAJIBU WAKO
Imeandaliwa na:
Jukwaa la Waislamu la Kuratibu Mabadiliko ya Katiba Tanzania (Juwakata)
Dar es Salaam,
Tanzania.
Twitter Bird Gadget