Monday, February 20, 2012

Amri ya kufuga ndevu!

Ndugu zangu waislamu, kufuga ndevu ni lazima(wajib) sio sunnah
Dalili katika Qur-aan tunaona kwamba hata mitume walikuwa wakifuga ndevu. Hii ni kauli ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) kuhusu Haaruun  ('alayhis-salaam alipomwambia Musa ('alayhis-salaam) alipomshika ndevu zake baada ya kuwaona wana wa Israaiyl wamepotoka: 
((Akasema: Ewe mwana wa mama yangu! Usinishike ndevu zangu, wala kichwa changu. Kwa hakika naliogopa usije sema: Umewafarikisha Wana wa Israil, na hukungojea kauli yangu))  [Twaaha 20:94]
Hapa tunakupa dalili zilizothibitika katika Sunnah:
1.    Mtawala wa Yemen, aliyechaguliwa na Mfalme wa Kiajemi Kisraa, alituma majumbe wawili kwa Mtume Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) kumpelekea mwaliko. Wakati hao walipotokezea mbele ya Mtume Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam), aliwaona hao wamenyoa ndevu na kufuga masharubu (ndevu za mdomo). Kwa hayo yeye alichukizwa kuwatazama hao (kwa sababu ya kuonekana visivyo sawa) na aliwaambia : "Ole wenu ! Je ni nani aliyewaambia kufanya hivyo ?"   Wao walimjibu: "Bwana wetu! (wakimaanisha Kisraa)." 
Mtume Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) aliwaambia: "Lakini Mola wangu, aliye Mkuu 
na Aliyetukuzwa, ameniamrisha mimi kuibakiza ndevu yangu peke yake na kunyoa masharubu yangu."  
[Imerekodiwa na Ibn Jarra-abar, na al-Albaaniy kuwa ni Hasan (nzuri) ]
2.    Mtume Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amewaamrisha wanaume wafuge ndevu peke yake. Hadiyth zifuatazo pia zina maana hizi hizi : "Nyoeni masharubu na muziache ndevu".[Al-Bukhaariy na Muslim]
3.    Mtume Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema:"Nyoeni masharubu yenu na muoteshe ndevu zenu. Muonekane tofauti na Wamajusi (wafuasi wa dini ya waabudu moto iliyokuwapo huko Uajemi [Iran]). [Muslim]
4.    Mtume Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: "Nyoeni masharubu yenu na kuziacha ndevu zenu peke yake. Muwe tofauti na Ahlul Kitaab (Mayahudi na Manaswara)." [Muslim]
5.    Mtume Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: "Muwe tofauti na  Mushrikiyn, mnyoe masharubu yenu na kufuga ndevu" [Al-Bukhaariy na Muslim]
Kwa kifupi hizi ni dalili chache kuonyesha Uwajibu wa jambo hilo, na vilevile ni maarufu kuwa Maimam Abu Haniyfah, Maalik, Ash-Shaafi'iy, Ahmad bin Hanbal na wengineo wamesema ni HARAAM kunyoa ndevu.
Na kwa kufahamu kuwa jambo hilo ni baya na ni ukiukwaji wa sheria ambayo imetoka kwa Muumba na kuthibitishwa kimaelekezo na kivitendo kwetu na Mjumbe Wake (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) ndio Maimaam hao wakatoa maamuzi yao katika suala hilo.
Amiyr Muadilifu 'Umar ibn 'Abdul-'Aziyz inasemekana katika vyanzo vya kihistoria kuwa alikuwa hakubali katika utawala wake ushahidi wa mtu mwenye kunyoa ndevu! Vilevile tunaona kwenye madhehebu mbalimbali za Kiislam, haruhusiwi mtu kuswalisha ikiwa haweki ndevu kutokana na jinsi walivyofahamu uzito wa jambo hilo na Uwajibu wake.
Na ndevu ni mashavuni na kidevuni, unapaswa kufuga ndevu zote na si kidevuni pekee ambazo zaitwa mzuzu na ukanyoa za mashavuni; utakuwa unafanya makosa; zote hizo ni ndevu, ama zilizoko juu ya mdomo wa juu ambazo ni masharubu, hizo zatakiwa kupunguzwa na zisiwe refu.

No comments:

Post a Comment

Twitter Bird Gadget