Wednesday, February 22, 2012

Khamenei:Thamani ya Mwanamke katika Uislamu

Kuwepo suala lililopewa jina la 'suala la mwanamke' katika jamii mbalimbali za mwanadamu ni ishara ya kuwepo aina ya upotofu, mtazamo finyu na ufahamu usiokuwa sahihi kuhusiana na masuala ya kibinadamu. 
Licha ya kuwepo hatua kubwa za kiutamaduni katika ulimwengu wa leo, lakini mwanadamu hajaweza kufikia njia sahihi na ya wazi kuhusu mwanamke na baadaye mwanamume. Kwa msingi huo, mwanadamu ameendelea kusumbuliwa na matatizo mengi ikiwa ni pamoja na misimamo mikali, ufahamu potofu, uonevu, dhulma na matatizo ya kinafsi. 

Katika kipindi cha miaka mingi sasa haki nyingi za wanawake zimepuuzwa katika utamaduni wa Ulaya na Marekani na sambamba na hayo, uhusiano usiokuwa na mipaka wa maingiliano ya kujamiiana umekuwa ukisisitizwa kwa jina la kumthamini na kumpa hadhi mwanamke. 

Misingi na thamani za utawala wa Kirumi ndio msingi na kigezo cha utamaduni na ustaarabu wa sasa wa Magharibi ambao tunaulaani kwa sababu ya kumdhalilisha sana mwanamke. 
Magharibi inampa hadhi na kumuheshimu mwanamke kwa shabaha ya kushibisha moja ya hulka chafu na matamanio ya kimaada ya mwanadamu tu, na kitendi hiki kinahesabiwa kuwa ni kumdunisha na kudhalilisha zaidi kiumbe mwanamke. 
Ayatullah Khamenei: Thamani ya Mwanamke katika Uislamu

Tatizo kuu la familia katika dunia ya leo linatokana na mtazamo usiokuwa sahihi kuhusu masuala ya mwanamke, uhusiano wa mwanamke na mwanamume na namna ya jinsi hizo mbili. Ujumbe wa wahyi na ufunuo ambao umekusanya masuala muhimu kuhusu mwanamke na mwanamume, unaonyesha njia sahihi kwa ajili ya kutatua matatizo hayo. Qur'ani Tukufu haitoi mawaidha matupu, bali inamfunza mwanamke malezi ya kimaanawi, ustawi na maendeleo yake kwa kutoa mifano ya mwanamke kigezo. 

Mtume Mtukufu alibusu mkono wa Bibi Fatima al Zahra (as) akiwa na imani kwamba ni mfano wa kuigwa wa mwanadamu kamili. Suala hili halipaswi kutambuliwa kuwa lilifanyika kwa sababu ya mapenzi ya baba kwa binti yake. 

Uislamu unamtazama mwanamke kwa jicho la ukamilifu wa kiroho na kibinadamu na msingi huu unapaswa kupewa umuhimu katika uchunguzi unaohusiana na utamaduni, masuala ya kijamii na malezi ya kielimu ya wanawake. 
Masua ya thamani za Uislamu yanapaswa kuhuishwa katika jamii yetu. Kwa mfano suala la vazi la hijabu ni suala la thamani za Kiislamu. Licha ya kwamba kadhia ya vazi la hijabu ni utangulizi wa mambo mengine ya juu zaidi, lakini kadhia hiyo yenyewe ni thamani ya Kiislamu. Tunashikamana vilivyo na vazi la hijabu kwa sababu kulinda vazi hiyo kunamsaidia mwanamke kufikia daraja za juu za kiroho na kimaanawi na kumuepusha na kuteleza katika matope yaliko katika njia yake. 


Kushikamana kwa wanawake na vazi la hijabu kunawasaidia katika juhudi za kufikia daraja za juu za ukamilifu wa kiroho na kuwakinga ili wasitumbukie katika mashimo yaliyoko njiani. Mijadala kuhusu vazi la mwanamke haipaswi kuathiriwa na hujuma za kipropaganda za Magharibi. Hata hivyo vazi la hijabu la mwanamke si aina ya chador peke yake, (vazi la hijabu linalovaliwa na wanawake wa Kiirani), lakini chador ndio aina bora zaidi ya vazi la hijabu na alama yetu ya kitaifa na haikwamishi shughuli za wanawake Waislamu katika masuala ya kisiasa, kijamii na kiutamaduni. 


Wanawake katika jamii yetu wanapaswa kutajirisha zaidi vipawa vyao vikubwa katika nyanja mbalimbali za sayansi na elimu kwa kuchunga na kuzingatia hadhi na thamani za kiroho. Wanapaswa kusoma na kufanya jitihada kubwa za kufikia daraja za juu za elimu na maarifa. Kuburutwa wanawake katika ufuska ni moja ya maafa ya kubakia nyuma katika medani ya elimu na maarifa. 
Familia ni taasisi ya kimaumbile na kimsingi ya mwanadamu na inapaswa kuwa msingi wa mipango yote inayohusiana na wanawake. Familia ni mahapa pa ustawi na kukua kwa hisia, na wanawake wenye utaalamu mbalimbali wanapaswa kuwa msingi wa familia na kuwa na nafasi muhimu kama utunzaji wa nyumba. 


Sehemu ya hotuba ya Kiongozi Muadhamu katika hadhara ya wajumbe wa Baraza la Utamaduni na Masuala ya Kijamii ya Wanawake na viongozi wa Kongamano la Kwanza la Vazi la Hijabu ya Kiislamu



Chanzo: http://abna.ir/data.asp?lang=17&Id=257277

No comments:

Post a Comment

Twitter Bird Gadget