Wednesday, February 22, 2012

JE! MUNGU NA YESU NI MMOJA?


Makanisa ya Kikristo yanafunza ya kuwa Yesu Kristo si kama kuwa ni Mwana wa Mungu tu, bali hakika ni Mungu khasa.  Baba, Mwana na Roho Mtakatifu ni mmoja.  Watatu katika mmoja, na mmoja katika watatu.  Wote ni wa milele, wote ni sawa.  Yesu ni Mungu, na Mungu ni Yesu. Hiyo ni imani ya Kikristo, ambayo inaaminiwa na karibu Wakristo wote.  Hebu tuifunue Biblia tutazame inasema nini katika jambo hili? 

Mt Paulo katika barua yake ya kwanza kuwapelekea Wakorintho aliandika:
Naam, na sisi tumeonekana kuwa mashahidi wa uongo wa Mungu; kwa maana tulimshuhudia Mungu ya kuwa alimfufua Kristo, ambaye hakumfufua, ikiwa wafu hawafufuliwi.
1 Wakorintho 15.15
Juu ya kuwa Paulo anaambiwa ya kuwa akiamini kuwa Masihi (yaani Kristo) na Mwenyezi Mungu ni kitu kimoja hapa anasema: "Tulimshuhudia Mungu ya kuwa alimfufua Kristo." Ikiwa Mungu kamfufua Kristo, hawawezi kuwa wote wawili hao ni mtu  mmoja. Mmoja alikuwa ni mtenda, mfufuaji, na wa pili alikuwa ni mtendwa, mfufuliwa. Kama Kristo ni Mungu mwenye uwezo wa kufufua basi maelekeo ni kusema: "Kristo kajifufua", sio kafufuliwa. Mwenye kufufuliwa ni mfu asiyejiweza kitu.
Katika kitabu cha Matendo ya Mitume inasimuliwa kuwa Mt Stefano alisema aliyoyaona yaliyo mbinguni. Alisema:
Tazama!  naona mbingu zimefunguka, na Mwana wa Adamu amesimama mkono wa kuume wa Mungu.
      Matendo 7.56
Mwana wa Adamu ndiye Yesu, na kwa jina hilo ndio mwenyewe akipenda kujiita, sio Mwana wa Mungu. Hapo basi huko mbinguni Stefano anasema anamwona Yesu kakaa mkono wa kulia wa Mungu. Mwenye kukaa mkono wa kulia wa fulani hawezi kuwa ndiye yule yule fulani. Hayo ni maelezo ya mbinguni.  Ni wazi basi kwa ushahidi wa Biblia kuwa Yesu hakuwa Mungu mbinguni kama alivyokuwa si Mungu duniani.
Yesu alipokimbilia kwenye Mlima wa Zaituni na huku akisakwa na Mayahudi alijitenga na wanafunzi wake.  Huko faraghani aliomba hivi:
Ee Baba, ikiwa ni mapenzi yako, uniondolee kikombe hiki; walakini si mapenzi yangu, bali yako yatendeke.  Malaika kutoka mbinguni akamtokea akamtia nguvu.
  Luka 22.42-43
Hapa tunaona mambo matatu muhimu:
  1. Yesu anamwomba Mungu. Yesu anamwabudu Mungu. Wawili hao ni mbali mbali, na vyeo vyao ni mbali mbali. Yesu ni mtumwa mnyonge mwenye kuomba na kuabudu. Na Mungu ni Mwenyezi Mungu mwenye uwezo wote na mwenye kustahiki kuabudiwa pekee, hata na Yesu, mwenye kutakiwa msaada pekee, hata na Yesu.
  2. Mapenzi ya Mungu ni mbali na yale ya Yesu. Yesu hataki kuuliwa, ananyenyekea na kuomba kwa Bwana wake: "uniondolee kikombe hiki" cha mauti.  Yesu hana azma hata chembe ya kufa msalabani, kifo cha mhalifu, kifo cha laana kama maadui zake  Mayahudi walivyoazimia kumpatilisha nacho. Lakini anakiri kuwa ni mapenzi ya Mungu sio yake yeye yatendeke. Yeye hana hila wala nguvu za kuzuia kudra ya Mwenyezi Mungu.
  3. Yesu, Mwana wa Adamu, anakata tamaa. Imani inampunguka. Kavunjika moyo. Ikabidi "Malaika kutoka mbinguni akamtokea akamtia nguvu."
Jee, yaelekea kuwa Yesu ndiye Mungu? Yaelekea kuwa yeye na Mungu kuwa ni sawa? Kama upo wasiwasi wo wote wa kujibu hayo, mwenyewe Yesu anajibu kama anavyo hadithiwa na Yohana kuwa kasema:
Baba ni mkuu kuliko mimi.
Yohana 14.28
Na mwishoni naye yupo mslabani:
Na kama saa tisa, Yesu akapaza sauti yake kwa nguvu akisema, Eloi, Eloi, lama sabakthani?  yaani, Mungu wangu, Mungu wangu, Mbona umeniacha?
Mathayo 27.46
Yafaa hapa tujiulize: Yesu akimlilia Mungu gani hapo msalabani ikiwa naye mwenyewe ni Mungu? Au nini alikusudia aliposema: "Mungu wangu naye ni Mungu wenu"?  Maneno hayo kama yanaonyesha cho chote basi yanaonyesha unyenyekevu wa Yesu mbele ya Mungu wake.  La kustaajabisha ni kule kukata tamaa kwake na kuvunjika moyo.  Huwaje mtu wa imani, licha ya nabii na mwana pekee wa Mungu, akate tamaa na rehema ya Mwenyezi Mungu.  Ama kuwa Mungu akate tamaa na Mungu, na kumyayatikia: "Mungu wangu, Mungu wangu, mbona umeniacha", ni jambo ambalo halimkiniki kuwa.
Kwa uthibitisho ulio wazi Biblia inatwambia kuwa Yesu si Mungu, wala Mungu si Yesu.

No comments:

Post a Comment

Twitter Bird Gadget