Wednesday, April 4, 2012

Ijue Jihadi



NINI JIHADI

Maana ya Jihadi tunaweza kuiangalia katika mtazamo wa kilugha na kisheria.

Lugha:  Neno Jihadi humaanisha juhudi au kujihimu na kustahamili taabu na        

              mashaka katika kufanya jambo au kutumia nguvu na uwezo katika kutimiza  jambo fulani.

Sheria:  Kujitolea na kupigana kuilinda dini ya Allah (Subhaanahu Wata’ala) na kulinyanyua neno lake na kuhakikisha kuwepo haki na uadilifu katika ardhi.

Ndani ya Quraan neno Jihadi limetumika mara nyingi sana kumaanisha wale wanaojitolea kwa ajili ya Allah (Subhaanahu Wata’ala). Kujitolea huku na kusimama kidete kuilinda dini ya Allah (Subhaanahu Wata’ala) kwa mapambano ya kivita ndio maana inayojulikana kila panapotajwa jihadi.

Jihadi ya nafsi ni kwa mja kuelekea kupigana na nafsi yake badala ya kupigana na maadui wa dini ya Allah (Subhaanahu Wata’ala). Wakati mwengine hutumika neno Tazkiya ikimaanisha kuitakasa. Pia neno Muhasaba (kuihesabu nafsi) hutumika na yote haya tutayajumuisha katika neno Jihadi.

Aina za Jihadi

1          Jihadi dhidi ya nafsi

Kupigana mja na nafsi yake inayoamrisha maovu kwa kuikatalia kila kitu ambacho inakitaka lakini Allah (Subhaanahu Wata’ala) pamoja na Mtume wake (Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam) amekikataza. Jihadi hii ni nzito na inahitaji subira na uvumilivu wa hali ya juu kwani Allah (Subhaanahu Wata’ala) anatubainishia katika Suuratu Nnaaziaat  40-41

        فَإِنَّ الْجَنَّةَ هِىَ الْمَأْوَى  وَأَمَّا مَنْ خَافَ مَقَامَ رَبِّهِ وَنَهَى النَّفْسَ عَنِ الْهَوَى

Na yule mwenye kuogopa kusimamishwa mbele ya mola wake na akaikataza nafsi na matamanio (yake) basi hakika pepo ndiyo makaazi yake.

Na hadithi ya Mtume (Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam) iliyopokelewa na Hakim, Attwabraaniy, Ibn Majah na Attirmidhiy

المجاهد من جاهد نفسه فى طاعة الله والمهاجرمن هاجرمانهى الله عنه            

“Mwenye kupigana Jihadi ni yule anaepigana na nafsi yake katika kumtii Allah (Subhaanahu Wata’ala) na mwenye kuhajiri ni yule aliyehajiri (aliyehama) yale aliyoyakataza Allah(Subhaanahu Wata’ala)”

Kwa hivyo pale tunapoelekea kwake na kumtii Allah (Subhaanahu Wata’ala) huku tukiwa na imani thabiti, mola wetu huturehemu kwa kutupatia kinga dhidi ya maovu na mambo machafu.

2          Jihadi dhidi ya Shetani

Kwa kwenda kinyume na kila mbinu na mikakati ya shetani alielaaniwa. Kwani shetani hukoroga mambo lisijulikane zuri na baya. Uzito wa Jihadi hii unazidi kwani adui mwenyewe hatumuoni lakini yeye anatuona hivyo hatuna uwezo wa kujua uwezo na nguvu zake ila yeye anatujua udhaifu wetu na matamanio yetu.

Allah (Subhaanahu Wata’ala) anasema katika Suuratu Nnuur /21

يأَيُّهَا الَّذِينَ ءَامَنُواْ لاَ تَتَّبِعُواْ خُطُوَتِ الشَّيْطَـنِوَمَن يَتَّبِعْ خُطُوَتِ الشَّيْطَـنِ فَإِنَّهُ يَأْمُرُ بِالْفَحْشَآءِ وَالْمُنْكَرِوَلَوْلاَ فَضْلُ اللَّهِ عَلَيْكُمْ وَرَحْمَتُهُ مَا زَكَى مِنكُم مِّنْ أَحَدٍ أَبَداً وَلَـكِنَّ اللَّهَ يُزَكِّى مَن يَشَآءُ  وَاللَّهُ سَمِيعٌ عَلِيمٌ    

“Enyi mlio amini! msizifuate nyayo za Shetani. Na atakaye fuata nyayo za Shet'ani basi yeye huamrisha machafu na maovu. Na lau kuwa si fadhila ya ِِAllah na rehema yake juu yenu, asingelitakasika miongoni mwenu kabisa hata mmoja. Lakini Allah humtakasa amtakaye, na Allah ni Mwenye kusikia, Mwenye kujua”

3          Jihadi dhidi ya makafiri

Ni kupigana vita vya silaha na wale wote wanaomkana Allah(Subhaanahu Wata’ala) na  kumshirikisha  na wanadhihirisha bayana uovu wao. Jihadi hii inawezekana kwa kushiriki katika mapambano yenyewe au kwa kuchangia kwa hali na mali kwa ajili ya Allah(Subhaanahu Wata’ala). Jihadi imetajwa katika sehemu nyingi katika Quraan kama Attahrimm /9

يأَيُّهَا النَّبِىُّ جَـهِدِ الْكُفَّارَ وَالْمُنَـفِقِينَ وَاغْلُظْ عَلَيْهِمْ وَمَأْوَاهُمْ جَهَنَّمُ وَبِئْسَ الْمَصِيرُ

Ewe Nabii! Pambana na makafiri na wanafiki, na kuwa mgumu kwao! Na makaazi yao ni Jahannamu. Na hayo ni marejeo mabaya

4             Jihadi dhidi ya wanafiki

Ni jihadi ya kujenga hoja dhidi ya wanafiki kwa kushikamana na dalili sahihi (Quraan na sunnah) hasa wakati wa fitna, majaribu na mitihani..Jihadi hii ni nzito kuliko zilizopita kwani inahusu watu ambao wapo miongoni mwetu na tunaishi nao lakini hatuwajui undani wao. Ingawa wanafiki ni wachache lakini sumu yao ni kubwa na binadamu hatuna haki ya kumtaja mja ni mnafiki (unafiki wa kiitikadi) kwani hilo analijua Allah (Subhaanahu Wata’ala) pekee. Tulichopewa sisi na alama tu. Anasema Allah (Subhaanahu Wata’ala) katika Al furqaan /20.

وَجَعَلْنَا بَعْضَكُمْ لِبَعْضٍ فِتْنَةً أَتَصْبِرُونَ وَكَانَ رَبُّكَ بَصِيراً  ….   

“…Na tumewajaalia baadhi yenu wawe ni majaribio kwa wengine; je! Mtasubiri? Na Mola wako  ni mwenye kuona.”

Adui huyu wa unafiki ambae hudhirisha uislamu lakini ndani ya nafsi yake ni kafiri (unafiki wa kiitikadi) silaha yake nzito ni  kuuvunja umoja na mshikamano wa umma wa kiislamu katika kufuata yale aliyotuachia Mtume wetu (Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam) Quraan na Sunnah ambazo moja kwa moja adui huyu huingiwa na khofu na woga kwani hatokuwa tena na mbinu za kuingiza fitna na uharibifu miongoni mwa waislamu.

NINI NAFSI

Nafsi nayo katika lugha ya kiarabu inaweza kutafsiriwa kwa maana tofauti zikiwemo roho, kiwiliwili, moyo, akili, uhai au dhati. (Muujam Kassis).

Hakuna maana kamili ya nafsi kisheria kwa mujibu wa maulamaa kwani kinachozungumzwa ni nafsi kama ilivyo. Hata hivyo baadhi ya wataalamu wa elimu ya nafsi wanasema:

Nafsi ya mtu ni kila kinachohusiana naye kama vile mwili wake, nguvu zake, nguo zake, nyumba yake, kazi yake na kila anachokimiliki.

Kwa hivyo nafsi ni kila kinachohusiana na mwili, kiroho na kijamii katika yaliyopita , yaliyoko na yatakayotokea kwani yote hayo yanaacha athari katika tabia na mwenendo wa mja.

Kuna kauli tofauti kuhusu nafsi na roho kwamba ni kitu kimoja au ni vitu tofauti.

Wapo maulamaa wanaosema kwamba nafsi na roho ni kitu kimoja yaani nafsi ndiyo roho na roho ndiyo nafsi.

 Lakini maulamaa wa kisunni wamekubaliana kwamba haya ni majina mawili yenye kumaanisha kitu kimoja na wala havina tofauti. Ukiangalia hata katika Quraan Allah (Subhaanahu Wata’ala) amevitumia katika aya tofauti kumaanisha kitu kimoja. Kwa mfano Al Mujaadalah/22

                      ...أُوْلَـئِكَ كَتَبَ فِى قُلُوبِهِمُ الإِيمَـنَ وَأَيَّدَهُمْ بِرُوحٍ مِّنْهُ     

“…Hao ameandika katika nyoyo zao Imani, na amewapa nguvu kwa Roho itokayo kwake…”

Labda tofauti iliyopo ni kimatumizi tu kwani mara nyingi roho ikiwa bado imo katika kiwiwiwili cha binadamu huitwa nafsi na pale itakapotoka kama ni roho.

Na tofauti nyengine kimatumizi ni pale nafsi hii ikiwa katika kiwiliwili cha binadamu huwa katika hali ya kutamani zaidi dunia na roho hutamani akhera. Ukiziangalia tofauti hizi utaona ni za kimtazamo na kimatumizi lakini nafsi ndio hiyo hiyo roho na roho ndio nafsi. Kwa lugha ya kiingereza roho hufahamika kama spirit na nafsi kama soul.

Na kuthibitisha haya zaidi ni hadithi mbili sahihi zilizopokewa na Muslim moja iliyotajwa na Abu Salamah (Allah amuwie radhi) na nyengine kutajwa na Abu Hurayrah (Allah amuwie radhi) zote zikielezea kitu kimoja lakini hadithi ya kwanza ya Abu salamah (Allah amuwie radhi) kuitaja kama ni roho na ya pili ya Abu Hurayrah (Allah amuwie radhi) kuielezea kama ni nafsi.

 Amesema Mtume Muhammad (Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam):

 “Macho huyafuata roho inapotolewa (kwa kuikodolea).”

Amesema Mtume Muhammad (Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam):

  “Huoni pale mtu anapokufa macho yako hutazama kwa utulivu?” Wakasema: “Ndio Ewe Mjumbe wa Allah”. Mtume Muhammad (Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam) akasema: “Hayo hutokea pale macho yanapoifuata na kuikodolea nafsi pale inapotoka.”

                                                                                               

 MAANA YA KUJITAKASA

Kujitakasa(Tazkiya) katika lugha ya kiarabu ina maana ya kujitoharisha.

Kiistwilahi ni kuiinua na kuitoharisha nafsi dhidi ya maradhi na maafa yanayoweza kuiharibu.

Kuitakasa nafsi ni lengo kuu la kila mchamungu kwani kutakasika huko ndio njia ya kupata uongofu na kushindwa kuitakasa nafsi ni sababu ya kuangamia. Na athari za kutakasika kwa nafsi hudhihiri katika mwenendo na akhlaqi za muislamu katika maisha yake ya kila siku.

MAANDALIZI

Kabla ya mja kuingia katika kazi hii ya Jihadi dhidi ya nafsi na kabla ya kuelewa aina za nafsi kwanza itambidi  mja ajiweke katika mazingira mazuri ya kukabiliana na kazi hii.Vyenginevyo kuna hatari kubwa ya kukosekana malengo na hivyo tija yake kuwa ni hasara badala ya faida kwa mja.

Mazingira au maandalizi yenyewe ni kama yafuatayo:

1             Awe na elimu

Ni wajibu kwa mja kwanza awe na elimu juu ya mfumo mzima wa jihadi ya nafsi ili aweze kujielewa ni kitu gani anachokihitajia na mbinu /mikakati gani itumike ili aweze kufanikiwa kwa uwezo wake Sub-hana kukifikia.

Anasema Allah (Subhaanahu Wata’ala) katika Suuratu Zzumar/9

قل هل يستوى الذين يعلمون والذين لا يعلمون       

Sema: Je wanaweza kuwa Salla Allahu ‘Alayhi Wasallama wale wanaojua na wale wasiojua?

2             Nia njema na safi

Ni lazima kwa mja kuwa na nia nzuri kabisa ya kumridhisha Allah (Subhaanahu Wata’ala) na kujikurubisha kwake kwani ikiwa nia iliyokusudiwa ni vyenginevyo basi malengo hayatofikiwa. Pia nia ndio msingi wa kutakabaliwa au kutokupokelewa amali zetu.

أَمِيرِ الْمُؤْمِنِينَ أَبِي حَفْصٍ عُمَرَ بْنِ الْخَطَّابِ رضى الله عنه   قَالَ: سَمِعْت رَسُولَ اللَّهِ صلى الله عليه وسلم    يَقُولُ: " إنَّمَا الْأَعْمَالُ بِالنِّيَّاتِ، وَإِنَّمَا لِكُلِّ امْرِئٍ مَا نَوَى، فَمَنْ كَانَتْ هِجْرَتُهُ إلَى اللَّهِ وَرَسُولِهِ فَهِجْرَتُهُ إلَى اللَّهِ وَرَسُولِهِ، وَمَنْ كَانَتْ هِجْرَتُهُ لِدُنْيَا يُصِيبُهَا أَوْ امْرَأَةٍ يَنْكِحُهَا فَهِجْرَتُهُ إلَى مَا هَاجَرَ إلَيْهِ" .

رَوَاهُ الْبُخَارِيُّ  وَ مُسْلِمٌ

Kutoka kwa Amiri wa Waumuni, Abu Hafs 'Umar Ibn Al Khattaab Allah amuwie radhi ambaye alisema : Nilimsikia Mjumbe wa Allah  akisema:

Vitendo vinategemea (vinalipwa kwa) nia na kila mtu atapata kwa mujibu wa kile alichokusudia.  Kwa hivyo yule aliyehama  kwa ajili ya Allaah na Mtume wake, uhamaji wake ni kwa ajili ya Allaah na Mtume wake, na  yule ambae uhamaji wake ulikuwa ni kwa ajili ya manufaa ya kidunia au kwa ajili ya kumuoa mwanamke (fulani)  uhamaji wake ulikuwa kwa kile kilichomuhamisha.

Imesimuliwa  Bukhari na Muslim. 

3             Awe na ikhlasi

Kwa sababu ikhlasi ndio roho ya ibada hivyo Jihadi hii  ikifanywa kwa ikhlasi ambayo maana yake kisheria ni “kuzisafisha amali zisichanganyike na malengo mengine zaidi ya kutaraji radhi za Allah(Subhaanahu Wata’ala)” Basi itaiepusha jihadi hii na riyaa(kujionesha). Mara nyingi mukhlis huwa hazinasibishi amali na nafsi yake bali huzirudisha kwa Allah (Subhaanahu Wata’ala) . Na pia mukhlis mara zote anapofanya amali hujiuliza kabla ya kuzitenda je. Ni kwa ajili ya Allah(Subhaanahu Wata’ala) au kwa ajili ya kitu chengine?

4             Kujitolea

Hii ni kazi nzito kwa hivyo mja atatakiwa kujitolea na kutovunjika moyo kwa kipindi chote na kujenga tabia ya kutokata tamaa kwa mitihani na majaribu yatakayomfika.

5             Kuwa mkweli

Ni lazima mja awe mkweli na nafsi kwanza na pia watu wengine na juu ya yote awe mkweli kwa Allah (Subhaanahu Wata’ala) na hasa kujitambua hali aliyo, mazuri na mabaya yake, udhaifu na uwezo wake n.k na kujikubali ndani ya nafsi jinsi alivyo.

6               Khofu na matarajio

Kwa mwenye kuingia kwenye jihadi hii basi ni lazima awe na khofu na adhabu ya Allah(Subhaanahu Wata’ala) na hapo hapo kuwa na matarajio na malipo mazuri aliyowaandalia waja wake wema.Al kahf /110

    َمَن كَانَ يَرْجُو لِقَآءَ رَبِّهِ فَلْيَعْمَلْ عَمَلاً صَـلِحاً وَلاَ يُشْرِكْ بِعِبَادَةِ رَبِّهِ أَحَدَا                                                                                 

….Mwenye kutaraji kukutana na Mola wake basi na atende vitendo vyema, wala asimshirikishe yeyote katika ibada ya Mola wake

Haya mambo yanakwenda sambamba na yanategemeana  kwani kufanya jambo bila ya nia njema kwa Allah (Subhaanahu Wata’ala) kunaitia hatarini amali hiyo kutokubaliwa na Allah(Subhaanahu Wata’ala). Pia Kutokuwa mkweli kwa nafsi kunaashiria kwa mja hayuko “serious” makini na analolifanya na pia amali kuweza kuingiwa na riyaa (kujionesha) au hata kukosa ikhlasi. Na mja akijaribiwa kidogo tu huvunjika moyo na kuacha kazi ya Jihadi.Na kukosekana kwa khofu na matarajio basi utendaji wa amali yoyote unakosa msukumo(motivation).

Imam Ibnul Qayyim ameigawa Jihadi ya Nafsi katika daraja nne pia nazo ni :

1             Kufanya juhudi na kujifunza mafundisho ya dini ya kiislam, dini ambayo ni ya haki na hakuna kufuzu isipokuwa kwa kushikamana nayo duniani na kesho tuendako akhera…

2             Kufanya juhudi katika kuyatekeleza yale aliyojifunza kwani elimu bila ya amali - ingawa haitomdhuru  ila - haimtonufaisha

3             Kufanya juhudi katika kufanya Daawah – kuwaita watu katika Uislamu na kuwafundisha dini vyenginevyo atakuwa miongoni mwa wenye kuficha yaliyoteremshwa na Allah (Subhaanahu Wata’ala) katika uongofu na ubainifu na hivyo haitomfaa elimu yake na wala haitomuokoa na moto.

4             Kufanya juhudi kwa kustahamili taabu na mashaka katika kufanya Daawah na kustahamili masimbulio na yote hayo ni kwa ajili ya Allah (Subhaanahu Wata’ala)

( angalia Zaadul Ma-aad vol. 3 ukurasa 9-11) 

No comments:

Post a Comment

Twitter Bird Gadget