Wednesday, April 4, 2012

Nini Nasiha au Nasaha



NINI NASIHA/NASAHA
Nasiha/Nasaha ni neno la kiarabu ambalo huitwa nasiha ingawa Kiswahili cha kileo inaeleweka zaidi kama  nasaha. Na maana yake kilugha ni ushauri wa dhati.
Kisheria ni ule ushauri wa dhati unaotolewa na muislamu kwa muislamu kwa ajili ya kuleta mabadiliko katika tabia na mienendo isiyo sahihi na kueleka katika tabia na mienendo iliyokuwa sahihi.
HUKUMU YAKE
Ni Fardhu kifayah (wakifanya baadhi ya waislamu huporomoka kwa wengine)
 عن تَمِيمِ بنِ أوْسٍ الدَّارِيِّ رضي اللهُ عنه: أَنَّ النَّبي صلى الله عليه وسلم قالَ:"الدِّينُ النَّصِيحَةُ". قُلْنَا: لِمَنْ ؟ قالَ: "للهِ، ولِكِتَابِهِ، ولِرَسُولِهِ، ولِلأَئِمةِ المُسْلِمِينَ، وعامَّتِهِمْ"
                                                                               
  رَوَاهُ مُسْلِمٌ
Kutoka kwa Tamim Ibn Aus Addaariy Allah amuwie radhi  amesema kuwa Bwana Mtume (Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam)  kasema:
Dini ni nasiha.  Tukauliza: Kwa nani? Akasema kwa Allaah , Kitabu chake, na Mtume wake , na kwa Viongozi wa Waislamu na watu wa kawaida
                                              Imesimuliwa na Muslim
Tunaona katika hadithi hii sahihi jinsi Mtume (Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam) alivyoielezea dini yote kuwa ni nasiha/nasaha. Hata Maulamaa wanasema nasiha ni moja katika mihimili mikuu ya dini ya kiislamu. Hivyo kwa kila muislamu mwenye kuamini kwa dhati katika nafsi yake ana wajibu wa kuyachukua maagizo haya ya Mtume (Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam) kwa kuyatekeleza kwa vitendo ilikuweza kujenga jamii ya kiislamu iliyo madhubuti.
Nasaha ni moja katika silaha bora kabisa katika Daawah. Lakini ikiwa mwenye kuitumia silaha hii hajajifunza vyema basi inawezekana ikaja kutumiwa visivyo na hivyo kuleta madhara  makubwa  na balaa badala ya faida.
MASHARTI YA KUTOA NASAHA
    1      NIA NJEMA
Ni wajibu wa kila muislamu anaetaka kupata radhi za Allah (Subhaanahu Wata’ala) kutia nia iliyokuwa safi kwa lengo la kutoa ushauri kwa ajili ya Allah(Subhaanahu Wata’ala). Kwa sababu ikiwa nia ya kuifanya amali hii ya kheri ni nyengine basi ndio pale madhara yanaweza kuja kutokea kwa mwenye kunasihi na mwenye kunasihiwa.
2      NASAHA IFANYWE KWA SIRI
Nasaha itabidi itolewe kwa faragha kati ya mwenye kunasihi na kunasihiwa . Hapa humsaidia mwenye kunasihiwa kutoathirika na mawazo na rai za watu wengine. Au kujiona kama amefedheheshwa na kuaibishwa mbele ya watu n.k Na pia mwenye kunasihi anapaswa pia kutunza siri za mwenye kumnasihi kama anavyotukumbusha Mtume (Salla Allahu’Alayhi Wasallam) katika hadithi:
                                                                   كفى بالمرء إثمًا أن يحدث بكل ما سمع"رواه مسلم.
“Yatosha kwa mtu kuwa dhambi ikiwa atalitangaza kila analolisikia”
                                                     Imesimuliwa na Bukhari
3     ITOLEWE KWA HEKIMA, BUSARA NA UPOLE
Mwenye kunasihi anatakiwa atumie busara na hekima wakati wa kunasihi.Kwa kufanya hivyo kuna uwezekano mkubwa wa kupata lengo lilikusudiwa kwani mwenye kunasihiwa inawezekana labda ameacha jambo ambalo Allah(Subhaanahu Wata’ala) amemtaka alitekeleze au  amefanya jambo ambalo Allah(Subhaanahu Wata’ala) amemkataza. Katika hali hii ya kuwa na majuto (guilty mind), ni hekima na busara pekee zitakazoweza kuufungua na kuulainisha moyo wa mwenye kunasihiwa.
Annahl /125
ادْعُ إِلِى سَبِيلِ رَبِّكَ بِالْحِكْمَةِ وَالْمَوْعِظَةِ الْحَسَنَةِ وَجَـدِلْهُم بِالَّتِى هِىَ أَحْسَنُ إِنَّ                         
                                                                   رَبَّكَ هُوَ أَعْلَمُ بِمَن ضَلَّ عَن سَبِيلِهِ وَهُوَ أَعْلَمُ بِالْمُهْتَدِينَ  
Waite waelekee kwenye Njia ya Mola wako Mlezi kwa hekima na mawaidha mema, na ujadiliane nao kwa namna iliyo bora. Hakika Mola wako  ndiye anaye mjua zaidi aliye ipotea Njia yake, na Yeye ndiye anaye wajua zaidi walio ongoka.
4    LENGO LIWE KUNASIHI NA SI KULAZIMISHA
Mwenye kunasihi ana wajibu wa kuhakikisha anatoa ushauri tu na hana jukumu la kumlazimisha anaempa nasaha  kwamba ni lazima ufuatwe. Kwa kufanya hivyo inakuwa si kunasihi tena bali ni kutoa amri ambayo inabidi itekelezwe. Ni vyema akautoa kwa ajili ya kumpa dira na muongozo katika kuelekea kwenye kheri na kupata radhi za Allah(Subhaanahu Wata’ala).
Albaqarah/256
لاَ إِكْرَاهَ فِى الدِّينِ قَد تَّبَيَّنَ الرُّشْدُ مِنَ الْغَيِّ فَمَنْ يَكْفُرْ بِالطَّـغُوتِ وَيُؤْمِن بِاللَّهِ فَقَدِ اسْتَمْسَكَ بِالْعُرْوَةِ الْوُثْقَى لاَ انفِصَامَ لَهَا وَاللَّهُ سَمِيعٌ عَلِيمٌ                                                                 
Hapana kulazimisha katika Dini. Kwani Uongofu umekwisha pambanuka na upotofu. Basi anaye mkataa shetani na akamuamini Allah bila ya shaka amekamata kishikio madhubuti, kisicho vunjika. Na Allah ni Mwenye kusikia, Mwenye kujua.
5     KUTAFUTA MUDA MUAFAKA WA KUTOA NASAHA
Wakati na muda ni jambo la kuzingatiwa sana kabla ya kutoa nasaha kwani ushauri unaweza kuwa mzuri lakini muda haukuwa muafaka na hivyo mwenye kunasihiwa kuweza kuukataa na kuutupilia mbali. Mtu anaweza katika hali ya hasira, kukerwa na kuwa na sababu itakayomfanya kutokuwa tayari kupokea lolote. Abdullah ibn Masoud, Allah Amuwie radhi, aliwahi kusema kwamba nyoyo mara nyengine huwa katika hali ya utulivu na kuwa tayari kusikiliza na wakati mwengine huwa katika hali ya kugubikwa na mambo. Hivyo nufaikeni na nyoyo katika hali za utulivu na kuziacha wakati zipo katika kugubikwa na mambo.
6     USHAURI/NASAHA  DHIDI YA DINI USIKUBALIWE
Kutoa ushauri mzuri ni moja katika sehemu ya dini yetu kwa mujibu wa hadithi ya Mtume (Salla Allahu ‘Alayhi Wasallam). Sasa ikiwa ushauri huu unatolewa kwa kufanya lililoharamishwa hii haitokuwa nasaha na wala si ushauri bali ni kupotosha.Kama kumshauri mwanamke kuvua Hijabu ili aweze kupata kazi, au kumhimiza  ndugu yako muislamu kusikiliza muziki na kadhalika

No comments:

Post a Comment

Twitter Bird Gadget