Saturday, April 21, 2012

Umuhimu wa Jihadi katika Uislamu


JIHAD maana yake ni juhudi. Dini maana yake ni mfumo au utaratibu wowote wa maisha. Uislamu maana yake ni kunyenyekea na kufuata sheria (utaratibu) ya Mwenyezi Mungu. Hivyo Jihad katika dini ya Uislamu ina maana ya juhudi au jitihada ya kuhakikisha utaratibu wa maisha (dini) ulioamriwa na Mwenyezi Mungu unafuatwa na wanaadamu.
Mujahidina ni wale watu waliokubali kufuata sheria za Mwenyezi Mungu (Waislamu) kisha wakafanya jitihada za kuwasaidia Waislamu wenzao (wanafiq) na wasio Waislamu ili nao wafuate utaratibu wa aliyewaumba kwa hiyari (mawaidha au mahubiri).
Wakuu wa Kanisa (wanatheolojia) wameviita vita vya Jihad kuwa ni "vita vitakatifu". Katika Biblia Takatifu Tabora (1967) ukurasa wa 430, wameandika maneno kwa herufi kubwa: "MATATHIA AANZISHA VITA VITAKATIFU". Wakifafanua zaidi chini yake wanasema" 2:1 Madhumuni yaliamsha ghafla moyo wa dini kati ya Wayahudi. 
Upinzani wa kukataa ustaarabu wa Wayunani uliambatana na vitendo vya kikatili (2:15-28) au kukaa tu kimya bila kufanya chochote cha kuupinga (2:15-28) au mwishoni vikazuka vita vitakatifu vinavyoazishwa na Matathia (2:39-48), vikaendelezwa hasa na Yuda Makabayo (5:3-5). Yuda Makabayo alifahamu kuwa kudumu kwa dini kuliungana na uhuru wa taifa. Kwa hiyo viliendelea hata kisha pata uhuru wa dini (6:57-62).
Hapa swali ni kuwa, "Kwa nini wakuu wa Kanisa wameviita vita hivi wakati vinadhuru (kuua, kujeruhi, kuharibu mali n.k.) maisha ya wanaadamu? Jibu tunalipata katika maneno ya Sheikh Matathia (r.l.) aliyeanzisha vita hivyo. Akiwausia wanawe anasema "msiyaogope maneno ya mtu mwenye dhambi, maana fahari yake itakuwa samadi ya funza. Leo atainuka, na kesho hataonekana kamwe, amerudia udongo wake na mawazo yake yamepotea. 
Basi ninyi, wanangu, muwe hodari, mfanye kwa kiume kwa ajili ya sheria, maana kwa hiyo MTATUKUZWA" (1 Makabayo 2:62-64).
Kwa mujibu wa maneno ya Sheikh Matathia (r.l.) tunaona kuwa cha muhimu kupigania ni sheria za Mwenyezi Mungu ili kuhakikisha wanadamu wote wanazifuata. Na kuwa utukufu wa Muislamu unapatikana pale tu anapopigania sheria za Mwenyezi Mungu. Aidha Sheikh Matathia alisema wazi kuwa endapo sheria za Mwenyezi Mungu hazitumiki, basi hakuna uhalali wa Muislamu yeyote kuwa hai. Ndio maana akasema: "... mbona basi tuzidi kuishi? Matathia na wanawe wakararua nguo zao wakajivika gunia. Wakalia kwa majonzi" (I Mak 2:13-14).
Labda swali la msingi hapa linaweza kuwa "kwa nini Mwenyezi Mungu analazimisha Waislamu wapiganie sheria za Uislamu tangu Agano la Kale (Torati) na Agano Jipya (Qur’an)?" Ili kupata jibu sahihi la swali hili, lazima turejee nyuma kabisa tujue hikma ya Mwenyezi Mungu ya kutuumba ili tujue kwa nini tupo hapa duniani.
Mwenyezi Mungu anasema: "Sikuwaumba majini na watu ila wapate kuniabudu". (Qur’an 51:56). Hapa tunaona kuwa, tumeumbwa ili tumwabudu Mwenyezi Mungu (s.w.). Ibada ni neno la Kiarabu lenye maana ya kutumika (servitude) kwa hiyo tumeumbwa ili tumtumikie Mwenyezi Mungu (s.w.). Kutumika maana yake ni kutii na kutekeleza chochote unachoamriwa na unayemtumikia. Hii ina maana kuwa tumeumbwa ili tumtii Mwenyezi Mungu kwa yote aliyotuamuru. 
Kwa hiyo kukataa au kusita kutekeleza chochote kilichoamriwa na Mwenyezi Mungu ni kwenda kinyume na maumbile. Hivyo inahitajika nguvu (jihadi ya mahubiri au vita) itakayomsaidia binaadamu ili arejee katika lengo lake halisi la kuumbwa. "Sikuwaumba majini na watu ila wapate kunitii". (Qur. 51:56)
Labda swali lingine muhimu sana hapa ni kuwa "kwa nini tulazimishwe kurejea kwa Mwenyezi Mungu?" Jibu liko wazi sana. 
Ukweli ni kuwa, binaadamu katika maisha yake yote duniani na akhera anatumia neema za Muumba wake. Iwe katika kumtii au kumuasi. Kwa mfano; mtu akihubiri dini anatumia akili, midomo, masikio, macho, mikono n.k., viungo ambavyo amepewa na Mwenyezi Mungu (s.w.). Kama ni mhubiri wa kweli atakuwa anatumia viungo hivyo kumtii Mwenyezi Mungu na akiwa mhubiri wa uwongo, atatumia viungo hivyo hivyo kudanganya, kupotosha, kutukana, kudhalilisha Mitume wa Mwenyezi Mungu n.k.
Hapo atakuwa anamwasi Mwenyezi Mungu na kuwaingiza watu motoni. 
Mfano mwingine ni kuwa, mtu akiamua kustarehe na mkewe au mumewe, watatumia viungo walivyopewa na Mwenyezi Mungu na watapata starehe waliyokadiriwa na Muumba wao. Hapo watakuwa wanamtii Mwenyezi Mungu (s.w.) na ni "sadaka". Lakini mtu huyo huyo akienda kuzini atatumia viungo vile vile alivyotolea "sadaka" na atapata starehe ile ile aliyoipata kwa mkewe au mumewe. Hapo anatumia neema za Mwenyezi Mungu kumuasi Mwenyezi Mungu. 
Hivyo hakuna wakati ambao binaadamu ataweza kutumia neema alizojitengenezea mwenyewe.
Na kwa kuwa neema zote (roho, viungo vya mwili, mali, nguvu, n.k.) tumepewa ili vitusaidie katika lengo letu la kuumbwa, yaani kumtii Mwenyezi Mungu, neema hizo ni haramu kuzitumia katika kumuasi Mwenyezi Mungu (s.w.).
Kwa kuwa Mwenyezi Mungu anatupenda sana viumbe wake, ndio maana akatuwekea mbinu mbalimbali za kutusaidia katukumbusha wajibu wetu. 
Binadamu tuko tofauti tofauti. Hivyo hata mahitaji yetu nayo ni tofauti tofauti. Kuna watu ambao hawahitaji "bakora" ili waishi kama apendavyo Mwenyezi Mungu. Hawa mawaidha, mahubiri, sala tano, saumu ya Ramadhani, zaka na hija vinawatosha kabisa. Kuna wale ambao bila "bakora" hawawezi kumtii Mwenyezi Mungu.
Hawa wanahitaji mawaidha, mahubiri, viboko 100 (wazinifu wasioona au kuolewa), kukatwa mikono (wezi), kupigwa mawe hadi wafe (wazinifu waliooa au kuolewa), kusulubiwa (majambazi n.k). Kila mtu lazima apewe mahitaji yake kamili na huo ndio uadilifu. 
Kumnyima au kumpunguzia mtu mahitaji yake ni kuvunja haki za binaadamu. Hivyo anayehitaji kupigwa viboko mia (mzinifu) lazima apigwe na anayehitaji kupigwa mawe hadi afe, lazima apewe haki yake. Kila mtu lazima apate haki yake aliyopewa na Muumba wake.
Hivyo, wakuu wa Kanisa wameviita vita vya Jihadi kuwa ni "vitakatifu" kwa kuwa vinarejesha heshima na utukufu wa mfalme wa mbingu na ardhi. Aidha, vinawasaidia wanaadamu walioghafilika na dunia kupatanishwa na Muumba wao. 
Watu wanaofanya jitihada (mujahidina) ya kuwapatanisha wanaadamu na Mwenyezi Mungu, wakuu wa Kanisa wamewaita "Watakatifu", kwa kuwa wamejitoa muhanga na kuhatarisha maisha yao ili wanaadamu wenzao waishi kwa kufuata sheria za Mwenyezi Mungu na sio sheria zilizotungwa na wanaadamu.
Ndio maana hata "somo" wangu Mtakatifu Bernardo (Mfaransa) alikuwa Mtakatifu sana na kupewa cheo cha "Doctor Mekifluus" japo ndiye aliyepewa jukumu na Pope la kupiganisha vita vya pili vya msalaba. Katika vita hivi Wakristo walishindwa vibaya sana, kwani walikuwa wanapigana na jeshi la Mwenyezi Mungu (Waislamu). Mtakatifu Bernardo alikufa Agosti 20, 1153.
Dunia na vyote vilivyomo ni mali ya Mwenyezi Mungu (s.w.). Mtawala yeyote katika sehemu yoyote ya dunia lazima atawale kwa kufuata utaratibu (sheria) uliowekwa na mwenye mali. 
Hivyo, mtawala (Rais, Mfalme, Sultan n.k.) anayetawala kinyume na mwenye mali (Mwenyezi Mungu) ameghafilika na dunia kwa kudhani ni yake. Kwa hiyo wanatakiwa Mujahidina wajitokeze na kumzindua kwa maneno (mawaidha/mahubiri) na wakiona hayamzindui, wamzindue kwa vitendo (vita vya jihad).
Waislamu ndio wamepewa jukumu la kuhakikisha dunia inaongozwa kama atakavyo Mwenyezi Mungu maana wakashushiwa ufunuo (Agano) mpya (Qur’an) na wakaongezewa tafsiri yake katika Sunna za Mtume Muhammad (s.a.w.). Makafiri hawana ufunuo toka kwa mwenye dunia, ndio maana kila kukicha wanahaha kubandika viraka kwenye miongozo yao (katiba). Kuishi kwa kufuata miongozo toka kwenye vichwa vilivyojaa "bingwa" na "safari" ni ukafiri (tazama Qur. 5:44, 5:49-50).
Ili kuwaepusha Waislamu Waislamu na ukafiri huo, Mwenyezi Mungu aliahidi toka katika Katiba ya Kale kuwaadhibu vikali Waislamu watakapokwepa wajibu wao. Anasema: "Naye BWANA atapiga Misri, akipiga na kuponya; nao wakirudi kwa BWANA atakubali maombi yao na kuwaponya". (Isaya 19:22). Kwa ufafanuzi zaidi, rejea makala yangu "Utabiri sahihi wa kuibuka kwa Uislamu" katika AN-NUUR Na. 171 Uk. 14.
Tangu zamani za Agano la Kale, Mwenyezi Mungu amekuwa "akiwachapa bakora" Waislamu (Wayahudi) kila wanapojisahau ili kuwakumbusha kuwa wao ni "TAA" ya dunia. Waislamu wenzetu wa zamani walizinduka haraka sana mara tu "wakichapwa bakora". Ndio mana viongozi wa Kanisa wanawasifu kwa kusema "Matathia aanzisha vita vitakatifu ...madhulumu yaliamsha ghafla moyo wa dini kati ya Wayahudi (Waislamu)... mwishoni vinazuka vita vitakatifu ... Yuda Makabayo alifahamu kuwa kudumu kwa dini kuliunganika na uhuru wa taifa (siasa). Kwa hivyo vita viliendelea hata kisha pata uhuru wa dini (6:57-62) Biblia Takatifu Tabora Uk. 530.
Sisi Waislamu wa sasa pamoja na "bakora" tunazochapwa Bosnia, Kossovo, Msikiti wa Uwanja wa Ndege Morogoro, Msikiti wa Mwembechai n.k. ndio kwanza tunageukia upande wa pili ili tuuchape usingizi sawa sawa. Mwenyezi Mungu hakati tamaa wala hashindwi kutuamsha kwenye usingizi wetu mnono. Hivyo tusubiri "bakora safi sana" ambayo kwa hiyo lazima tutazinduka.
Na Bernard P. Nyangasa

No comments:

Post a Comment

Twitter Bird Gadget